24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

UMRI WA MADAKTARI, MAPROFESA KUSTAAFU WAONGEZWA

Na MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM


SERIKALI imefanya marekebisho ya utumishi wa umma sura 298  kuongeza umri wa kustaafu kazi maprofesa na wahadhiri waandamizi katika vyuo vikuu vya umma.

Wengine watakaohusika ni  madaktari bingwa wa magonjwa ya binadamu katika hospitali za umma nchini.

Hiyo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa   jana ambayo imesainiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa  Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Makwaia Makani.

Taarifa hiyo inasema  umri wa kustaafu kazi kwa madaktari katika hospitali za umma ni miaka 60 badala ya 55 kwa hiari na miaka 65 badala ya 60 kwa mujibu wa sheria.

“Katika kukabiliana na upungufu wa wanataaluma na wataalamu waliopo kwa sasa katika vyuo vikuu vya umma na hospitali za umma nchini.

“Serikali imefanya marekebisho katika sheria ya utumishi wa umma sura 298 kuongeza umri wa kustaafu kazi maprofesa na wahadhiri waandamizi katika vyuo vikuu vya umma na madaktari bingwa wa magonjwa ya binadamu katika hospitali za umma kupitia sheria ya marekebisho ya sheria mbalimbali Namba 1 ya Mwaka 2008.

“Marekebisho yaliyofanywa katika sheria ya utumishi wa umma yameainisha umri wa kustaafu kazi kwa kada tajwa hapo juu kwa miaka 60 badala ya 55 kwa hiari na miaka 65 badala ya 60 kwa mujibu wa sheria. Mabadiliko haya yameanza rasmi Februari 9 mwaka huu,”ilisema sehemu ya taarifa hiyo.

Taarifa hiyo ilisema madaktari bingwa wote ambao hawakuwa wamefikisha umri wa kustaafu kazi kwa mujibu wa sheria Februari 9 mwaka huu, wataendelea na ajira zao hadi hapo watakapofikisha miaka 65 na kwamba taarifa zao za kustaafu kwa wale waliopata zinafutwa.

Vilevile taarifa hiyo  ilieleza kuwa madaktari bingwa watakaotaka kustaafu kwa hiari watatoa taarifa ya maandishi kwa mkurugenzi mtendaji.

Alipoulizwa kuhusu taarifa hizo, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Umma na Huduma kwa Wateja, Aminiel Aligaesha alisema ni kweli tangazo hilo ni la kwao.

Kuanza kwa sheria hiyo kunatokana na kupitishwa  Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali Namba Tano wa Mwaka 2017 ambao utazihusisha sheria tano ikiwamo ya Utumishi wa Umma sura namba 298 ambako kifungu kipya cha 25A kitaongezwa.

Vikao vya kamati za Bunge vimeanza huku miongoni mwa miswada itakayojadiliwa ikiwa ni ule utakaoongeza umri wa kustaafu kwa lazima kutoka miaka 60 hadi 65 kwa maprofesa, wahadhiri waandamizi na madaktari bingwa wa magonjwa ya binadamu wa umma.

Inaelezwa kuwa lengo la kuongezwa kwa sheria hiyo ni kuweka kwenye masharti ya umri wa kustaafu kwa watumishi wa umma ambayo hayapo kwenye sheria ya sasa.

Mfumo huo mpya unalenga kuongeza umri wa kustaafu wa utumishi wa umma kwa ridhaa kwa maprofesa na wahadhiri waandamizi wa vyuo vikuu vya umma na madaktari bingwa wa magonjwa ya binadamu wa hospitali za umma ili uwe 60 kwa wale wanaostaafu kwa hiari badala ya 55 wa sasa.

Pia, mfumo huo unalenga kuongeza umri wa kustaafu kwa lazima uwe miaka 65 badala ya sasa wa miaka 60 ya sasa.

“Marekebisho haya yanalenga kutekeleza uamuzi wa Serikali unaolenga kuongeza umri wa kustaafu kwa maprofesa, wahadhiri waandamizi wa madaktari bingwa wa binadamu kutoka vyuo vikuu vya umma na hospitali za umma,” ilielezwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles