27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Ulevi, matumizi ya dawa vyatajwa chanzo ugonjwa wa presha ya macho

Na AVELINE KITOMARY, DAR ES SALAAM

WAKATI jana dunia ikiadhimisha siku ya presha ya macho, unywaji pombe uliokithiri na matumizi mabaya ya dawa za macho, yametajwa kuwa chanzo  kikubwa cha ugonjwa huo.

Sababu zingine zilizoainishwa ni zile za umri mkubwa kuanzia miaka 40, kurithi,uvutaji sigara uliokithiri na ugonjwa wa kisukari.

Akizungumza jana wakati wa zoezi la upimaji wa macho katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili –Mloganzila, ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha siku ya presha ya macho duniani ambayo huwa ni kila Machi 7, daktari bingwa wa magonjwa ya macho, Dk Catherine Makunda, alisema ugonjwa huo unaendelea kuongezeka ambapo katika kliniki moja kwa wiki, huona wagonjwa 20 hadi 25.

“Leo tunafanya upimaji wa shikizo la macho kama sehemu ya kuadhimisha siku ya presha ya macho duniani, tunapima na wale wanaohitaji matibabu wanapewa dawa, tunatoa huduma bure na toka asubuhi tumeshapima wagonjwa 65 kati ya yao tisa wamekutwa na tatizo hilo, kwa leo tunatarajia kupima watu 300.

“Kwa umri tatizo linaanza ukiwa mzee ambapo chujio la maji linachoka, matumizi ya baadhi ya dawa za macho ambazo zilishakaa mda mrefu mfano ndugu yako alikuwa anatumia hiyo dawa na wewe ukatumia kuna zingine zinamadhara, nawashauri watu wasipende kwenda dukani kununua dawa bila kuwaona wataalamu,”alisema Dk Makunda.

Alisema pia wagonjwa wa presha ya jicho wanakumbana na unyanyapaa katika jamii zao hali inayosababisha kukata tamaa ya matibabu.

“Unyanyapaa upo, utakuta mwenye tatizo hana hata mtu wa kumsindikiza hospitali, kwahiyo kufatilia matibabu inakuwa ni shida na wagonjwa wengine wameacha matibabu kwasababu hiyo”alisema.

Alisema presha ya macho ni  ugonjwa unaoshambulia mfumo wa jicho ambapo presha inatakiwa iwe kati ya 10 na 20  inapozidi hapo inakuwa ni ugonjwa.

Aidha alisema tatizo la presha ya macho kwa watoto linasababishwa na maumbile ya kuzaliwa ingawa idadi yao ni ndogo.

Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Macho, Judith Mwende, aliwahimiza madereva kupima afya ya macho kabla ya kuendesha gari.

Naye Mfanyakazi wa Kampuni ya Salama Pharmaceutical, Nashron  Daniel, alisema wanasambaza dawa bure kwa lengo la kuadhimisha siku hiyo ili kusaidia jamii.

“Tumeamua kuungana na Mloganzila ili kufanya zoezi hili, kampuni itatoa dawa bure nawashauri watu wajitokeze kwa wingi inapotokea fursa kama hii,”alishauri.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles