24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Ukimwi bado tishio kwa Vijana-Serikali

Na Ramadhan Hassan,Dodoma

Utafiti unaonesha katika watu 72,000 wanaopata maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi kwa mwaka, asilimia 40 ni vijana na kati yao asilimia 80 ni Wasichana wenye umri kati ya  miaka 15-24.

Hayo yamebainishwa leo, Alhamisi April 29, jijini Dodoma na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Vijana, Patrobas Katambi wakati akifungua mkutano wa mwaka wa wadau unaotekeleza afua za VVU na Ukimwi zinazowalenga wasichana balehe na wanawake vijana.

Katambi amesema  kwa mujibu wa utafiti wa  mwaka 2016-2017  unaonesha katika watu 72,000 wanaopata maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi kwa mwaka asilimia 40 ni vijana na kati ya  hao asilimia 80 ni wasichana wenye umri kati ya  miaka 15-24. 

“Hii ina maana kuwa katika kundi la vijana 10 walioathirika wanawake ni nane hivyo sisi tukiwa kama vijana tunatakiwa kuliangalia jambo hili kwa umakini hali kwa wasichana sio nzuri,”amesema. 

Pia, amesema kiwango cha ushamili kimeendelea kupungua sambamba na kiwango cha maambukizi mapya na vifo vitokanavyo na ukimwi.

Amesema wastani wa kitaifa wa ushamili wa VVU ni asilimia 4.7 ambapo mkoa wa Njombe umekuwa kinara kwa kuwa na asilimia 11.4 ukifuatiwa na Mikoa ya Iringa asilimia 11.3,Mbeya asilimia 9.3.

Amesema kwa Mkoa wa Dodoma maambukizi yameongezeka kutoka asilimia 2.9 hadi kufikia asilimia 5.

Kutokana na hali hiyo, Katambi amesema Serikali itaendelea kuhakikisha inatoa fedha kwa ajili ya vijana huku akiwataka  kuchangamkia fursa za mikopo zinazotolewa katika Halmashauri nchini.

Naye,Mkurugenzi Mkuu Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania (TACAIDS), Dk.Leonard Maboko amesema lengo la kikao hicho ni kuwaleta wadau na kuona wamefikia wapi na wamekutana na changamoto zipi pamoja na kuzitatua.

“Sisi TACAIDS kazi yetu ni kuratibu na ndio maana hapa kuna taasisi kazi yetu kubwa ya hili kundi ni kuratibu kila mwaka hivyo hichi kikao ni cha kuwaleta hawa wadau kuona wamefikia wapi na wamekutana na changamoto zipi pamoja na kuzitatua,ili kujadiliana tulipotoka tulipo na tunapoelekea,”alisema Maboko.

Amesema Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa aliagiza Tacaids ifanye kazi na vijana ambapo alidai kwa sasa wanafanya kazi nao hususan wasanii.

Alisema takwimu zinaonesha vijana ni kundi lenye Changamoto katika maambukizi ya Ukimwi.

“Tulianzisha Kijiji Maalim kwa vijana ambayo inalenga masuala ya vijana na haya yote yalikuwa ni maagizo ya Waziri Mkuu na yalitokana na 

“Maambukizi mapya asilimia 40 yalikuwa yanatokea kwa vijana lakini asilimia 80 ya hao vijana ni wa kike,kwa umaalumu kabisa ndio maana hili kundi likapewa msisitizo huu.Takwimu zilituonesha hivyo tukaona  kuna haja ya kuweka mkazo katika hili,”alisema.

Kwa upande wake,Balozi Mwakilishi wa wasichana balehe na wanawake vijana,Rosemari Shani akisoma risala alisema wanakabiliwa na changamoto za  upungufu wa vituo vya kutolea huduma kwa vijana,ukosefu wa soko la uhakika wa bidhaa wanazozalisha,uelewa mdogo wa jamii kuhusu kinga za VVU.

“Elimu zaidi iendelee kutolewa tunaomba  uziimize Halmashauri ziendelee kutoa mikopo kwa wanawake.Sisi Kama wasichana tunakuahidi kufanya juhudi kujiunga na Veta na Sido ili kukuza ujuzi.Tutaendelea kuwajibika katika familia zetu,”alisema.

Alisema wanajivunia kumpata Rais mwanamke,Samia Suluhu Hassan kwani hiyo ni chachu kubwa kwao kuendelea kusoma na kufanya kazi kwa bidii.

“Tunajivunia kumpata Rais mwanamke jambo hili ni chachu kubwa kwetu.Tunaishukuru Serikali na wadau ambao wanatusaidia tunatarajia mambo mazuri,” amesema.

Kauli mbiu katika mkutano huo ilikuwa ni ‘Pamoja haina kufeli’

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles