27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Ujumbe wa China wasaka fursa nchini

ANDREW MSECHU-DAR ES SALAAM

UJUMBE kutoka Jimbo la Zhejiang nchini China, uko nchini kusaka fursa za uwezkezaji, ikiwamo kukutana na wafanyabiashara wakubwa watakaoweza kushirikiana nao katika uwekezaji maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza katika mkutano wake na wanahabari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa ujumbe huo, Ge Huijun, alisema hatua hiyo inatokana na ushirikiano wa China na Tanzania, ambao umezidi kuimarishwa siku za hivi karibuni.

Alisema jimbo la Zhejiang lenye zaidi ya wakazi milioni 57 lina fursa nyingi za biashara na uwekezaji, lakini pia lina wakazi wengi wenye uwezo wa kuwekeza nje ambao nao wanahitaji kujua fursa zilizopo Tanzania.

 “Kwa hiyo tumefika hapa kuunganisha wafanyabiashara na wawekezaji wa pande hizi mbili, ili wafahamishane fursa na maeneo wanayoweza kushirikiana katika uwekezaji kutoka pande zote.

 “Lakini pia jimbo letu la Zhejiang lina watu wengi ambao wana kipato cha kati na wanahitaji kutalii, kwa hiyo tulishatambua fursa za utalii zilizopoTanzania na tayari tulishaanzisha kampeni maalumu ya ‘Travel to Tanzania’ yenye uwezo wa kuleta hadi watalii milioni saba kwa mwaka,” alisema.

Alisema kupitia kampeni hiyo ya kuwataka watu wao wasafiri na kuja Tanzania kutalii, mapokeo yamekuwa mazuri na katika safari za awali zimetimiza zaidi ya asilimia 80 ya matarajio yao.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba Kabudi, alisema ziara hiyo ya ujumbe maalumu kutoka Zhejiang itaimarisha upatikanaji wa mitaji ya uwekezaji na uuzaji mazao nje, kwa kuibua soko jipya la wazalishaji kutoka nchini.

Profesa Kabudi alisema hiyo ni sehemu ya fursa muhimu kwa wazalishaji wa bidhaa za mashambani nchini, ambao sasa wanatakiwa waangalie soko la zaidi ya watu bilioni moja walioko China.

Alisema Jimbo la Zhejiang ni la nne kwa ukubwa nchini China likiwa na soko la zaidi ya watu milioni 57, likiwa na sifa kuu ya uzalishaji samaki, mchele, chai na hariri.

 “Kwa hiyo tuna nafasi ya kujifunza namna wao wanavyozalisha na kujua wanapungukiwa wapi, kisha kuwasaidia kujazia pale palipopungua.

“Lakini pia tunatakiwa kujua wana fursa za utaalamu kuhusu utalii, utaalamu kwenye ufundi stadi, ujenzi wa maeneo maalumu ya viwanda, uongezaji wa thamani kwenye mazao na kujifunza kwao kuhusu uvuvi wa kisasa,” alisema Profesa Kabudi.

Alisema wakati ujumbe huo ukikutana na wafanyabiashara jana, siku moja baada ya kutembelea na kukutana na wafanyabiashara wa Zanzibar juzi, Serikali inaendelea kusisitiza uwekezaji baina ya watu kutoka China na Tanzania, ili kuimarisha na kuboresha ukuaji wa uchumi

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles