27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Uhuru Kenyatta ang’ara Afrika

Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta
Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta

WASHINGTON, Marekani

RAIS wa Kenya, Uhuru Kenyatta, amewapiku marais wenzake wa Afrika Mashariki kwa kushika nafasi ya kwanza kwa ufanisi wa kazi, kwa mujibu wa utafiti wa Shirika la Gallup la nchini Marekani.

Utafiti huo ulitolewa jana ambapo licha ya Rais Kenyatta kuwa madarakani kwa kipindi cha mwaka mmoja ameweza kuwapiku wenzake waliodumu madarakani kwa muda mrefu.

Pamoja na Rais Jakaya Kikwete, kuingoza nchi kwa mwaka wa tisa sasa utafiti huo umeshindwa kumpa nafasi ya ushindi kati ya viongozi wenye uwezo kwa nchi za Afrika kutokana na juhudi za Tanzania katika kutafuta amani katika nchi za maziwa makuu.

Rais Kikwete aliibuka kwa kushika nafasi ya tisa sawa na asilimia 59 ya kura zilizopigwa kwa viongozi 10 wa nchi za kusini mwa  Jangwa la Sahara.

Katika utafiti huo, Rais Yoweri Museveni wa Uganda anayeiongoza nchi hiyo kwa miaka 27 alishika nafasi ya pili Afrika Mashariki na nafasi ya tisa Afrika kwa kupata asilimia 62.

Rais Kenyatta aliyeshika nafasi ya kwanza eneo hilo alikuwa watatu Afrika, kwa kupata asilimia 78, nyuma ya marais Ibrahim Boubacar Keita wa Mali na Ian Khama wa Botswana, walioorodheshwa wa kwanza na pili kwa kupata asilimia 86 na 81.

“Marais kutoka ukanda wa kusini mwa Jangwa la Sahara Afrika kwa zaidi ya nusu ya mataifa yaliyotathminiwa walipata zaidi ya asilimia 50. Mbali ya hayo, wengi wa marais hao ni miongoni mwa wanaohudhuria Kongamano la Viongozi wa Afrika nchini Marekani wiki hii,” ulieleza utafiti huo.

Kwa mujibu wa utafiti huo, Rais Joseph Kabila wa DRC Kongo, alikuwa wa mwisho kwa kupata asilimia 24 akifuatiwa na Rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma aliyepata asilimia 41.

Rais Kenyatta alifuatiwa na Rais mkongwe wa Cameroon, Paul Biya, aliyepata asilimia 70.

“Miongoni mwa viongozi waliopokea kiwango kikubwa cha kukubalika mwaka 2013, wachache wamekuwa madarakani kwa zaidi ya miongo miwili vile kama Biya na Museveni,” Gallup ilieleza.

Utafiti huo wa Gallup unaonyesha kuwa marais wengi waliopata alama nyingi walikuwa wamehudumu kwa vipindi vichache uongozini kama vile Ibrahim Boubacar Keita wa Mali.

Kutokana na hali hiyo utafiti huo uliofanyika Desemba mwaka jana huenda ukazua mijadala mbalimbali, ikizingatiwa kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja Kenyatta akiwa madarakani, Serikali yake ya  Jubilee imekuwa ikikabiliwa na mlolongo wa changamoto kadhaa ikiwemo viongozi wake kukabiliwa na kesi katika Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC) nchini Uhalanzi.

Changamoto kubwa zaidi ni ukosefu wa usalama katika eneo la Pwani, hali ambayo imechangia kudorora kwa sekta ya utalii.

Utafiti ulionyesha kuwa watu wengi waliozidi miaka 45 ndio walikuwa wakiunga mkono zaidi utendakazi wa rais huyo.

“Hali hii ni kinyume na nchini Nigeria, ambako watu wengi walio chini ya miaka 45 ndio waliunga mkono utendaji kazi wa Rais Goodluck Jonathan,” ulisema.

Shirika hilo ambalo lina makao yake mjini Washington, lilitoa takwimu hizo huku kongamano la viongozi hao na Marekani likitarajiwa kuangazia uimarishaji wa ushirikiano wa kiuchumi kati yake na bara Afrika ili kukabili tisho la China.

Katika kujumuisha takwimu hizo, shirika hilo lilisema kuwa liliwahoji watu 1,000 wa miaka 15 na zaidi katika mataifa husika.

Vigezo vingine vilivyozingatiwa ni uthabiti wa kisiasa katika mataifa husika kigezo kilichotajwa kuwa msingi mkuu wa ukuaji wa kiuchumi.

- Advertisement -

Related Articles

5 COMMENTS

  1. Nampongeza Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya, kwa bidii yake ya utendaji wa majukumu yake. Tunaomba na viongozi wetu wa Tanzania waige mifano yao kama Raisi Yoweri Museven wa Uganda pia.

  2. Inashangaza na kusikitisha kumwona raisi wetu akishika mkia katika utafiti huo. Hapa nchini tunamwona raisi wetu kama star katika Africa. Kumbe hapana. Utafiti huu unapaswa kutupa changamoto. Hivyo ndivyo tunavyoonekana mbele ya macho ya kimataifa.

  3. Sasa ni nchi gani duniani mtoto wa kidato cha kwanza ambaye amechaguliwa na wizara kuwa kashinda mtihani lakini hajui kusoma na kuandika kwani inajulikana wanafunzi 5000 nchi nzima walichaguliwa na kuingia kidato cha kwanza mwaka jana/juzi wakati hawajui kusoma na kuandika. Dunia inayaona. Je mtoto kutoka darasa la saba Tz anaweza kuingia kidato cha kwanza kule Kenya au Uganda,Malawi kama ilivyokuwa miaka ya 60, 70 na 80!!!!!!!

  4. Kuwa na bidii peke yake sio hoja kwani rais wetu Jakaya Mrisho Kikwete ni mwenye bidii kuliko wote Afrika ya Mashariki. Tofauti ni kwamba Uhuru Kenyata ametulia nyumbani akishirikiana na serikali yake na wakenya wenzake kwenye harakati za kukabiliana na vikwazo na kubuni majibu sahihi yatakaliwezesha taifa la Kenya liweze kusonga mbele kiuchumi kutokana na juhudi za wakenya wenyewe wakati Jakaya Mrisho Kikwete akiwa safarini nchi za ngambo muda mwingi akisaka misaada ya hali namali kwenye harakati za kukabiliana na vikwazo dhidi ya maendeleo ya taifa lake kiuchumi. Uhuru Kenyata amepata mafanikio makubwa ya kiutendaji kutokana na hulka aliyo nayo ya kupenda zaidi kujitegemea kwenye harakati zake za kulitafutia taifa lake maendeleo.

  5. Wakati serikali ikiunda baraza uwezeshaji kuwezesha wananchi kupitia sekta binasfi watu wengi walifurahi sana. Lakini badala ya kuwawezesha wafanyabiashara wa kati wanpeleka mabilioni ya kikwete kwa wauza magenge ya nyanya, Nazi na vitunguu. Hawa watatengeneza ajira kwa watanzania wangapi. Katika nchi zingine startup yoyote inayolenga kutengeneza ajira kwa watanzania iansaidiwa kwa fedha, ushauri na network. Hapa ni kinyume wanaona kwa nini UTOKE. Wanasaidia wasukuma mikokoteni.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles