23.3 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

UGONJWA WA MIHOGO WAWATESA WATAFITI

Na MWANDISHI WETU- DAR ES SALAAM


UGONJWA wa batobato na michirizi ya kahawia unaoshambulia mihogo unawatesa wataalam wa mazao kwa kuwa unaathiri mihogo.

Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na Mwanasayansi Mwandamizi aliyeko katika Kituo cha Kimataifa cha Utafiti wa Mazao cha IITA, James Legg, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za kituo hicho, jijini Dar es Salaam.

Legg aliyasema hayo wakati taasisi hiyo ilipokuwa ikiadhimisha miaka 50 tangu ilipoanzishwa.

“Kuna magonjwa mawili ambayo ni batobato na michirizi ya kahawiya ambayo yanasumbua sana wakulima wa mihogo katika Kanda ya Ziwa na kwingineko wanakolima mihogo.

“Kimsingi, magonjwa hayo ni hatari kwani yanaathiri mihogo na kushusha uzalishaji kwa kiasi kikubwa.

“Kutokana na madhara ya magonjwa hayo, Serikali na sisi kama wataalam wa utafiti wa mazao, tumekuwa tukifanya kila tunaloweza katika kuhakikisha tunajua chanzo hasa cha magonjwa hayo na namna ya kuyadhibiti ili yasiendelee kuleta madhara kwa wakulima,” alisema Legg.

Naye mtafiti mshiriki wa taasisi hiyo, Jacob Njela, aliwataka wananchi wawe na kawaida ya kupima mahindi, maharage na mazao mengine yenye sumu kuvu ili kuepuka madhara ya sumu hiyo.

“Sumu kuvu ni kama ukungu unaokuwa kwenye mazao kama mahindi na ina madhara makubwa pindi inapoigia katika mwili wa binadamu.

“Baadhi ya madhara yanayotokana na sumu hiyo ni magonjwa ya ini, figo, macho na magonjwa ya tumbo.

“Ili kuepuka sumu hiyo, kuna haja kwa wananchi kupima mahindi pindi wanapoyanunua kwa sababu sumu hiyo ina madhara makubwa mwilini na wakati mwingine inaweza kusababisha kifo,” alisema Njela.

Kwa upande wake, Fedrick Baijukya ambaye ni mtafiti aliyeko katika maabara ya udongo kituoni hapo, aliwataka wakulima wawe na kawaida ya kuwasiliana na maofisa ugani ili waweze kuwasaidia namna ya kuboresha kilimo chao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles