23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

UCSAF kunufaisha vyombo vya mawasiliano

Na Allan Vicent, Tabora

Wadau wa Mawasiliano hapa nchini wakiwemo wamiliki wa redio, luninga na huduma za waya (cable tv) wametakiwa kuchagamkia fursa zinazotolewa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) ili kuboresha usikivu wa vyombo vyao.

Wito huo umetolewa jana na Ofisa wa Mfuko huo Mhandisi Richard Sotery katika semina ya siku moja ya Wadau wa Mawasiliano kutoka Kanda ya Kati Mikoa ya Singida, Tabora na Kigoma iliyofanyika jana mjini hapa.

Alisema mfuko huo ni muhimu sana kwa watoa huduma za mawasiliano hapa nchini hususani redio za kijamii na watoa huduma za waya kwa kuwa umelenga kuweka usikivu katika maeneo yote ikiwemo vijijini.   

Alibainisha kuwa usikivu wa redio za kijamii katika maeneo mengi hapa nchini sio mzuri hivyo akatoa wito kwa wamiliki wa vyombo hivyo kushirikiana na mfuko huo ili kutimiza azma zao za kuanzishwa vyombo hivyo.

Mhandisi Sotery alifafanua kuwa serikali iko tayari kushirikiana na watoa huduma za mawasiliano ndiyo maana imeanzisha mfuo huo ili kuwawezesha kuboresha  vyombo vyao ili viwe na usikivu katika maeneo yote.

‘Mradi huu ni fursa muhimu kwa wadau wa mawasiliano hususani wamiliki wa redio za kijamii na watoa huduma za waya (cable tv), tunaomba ushirikiano wenu ili kunufaika na fursa za uwezeshwaji kupitia mradi huo’, alisema.

Kwa upande wake Ofisa wa Mfuko huo Mhandisi Shirikisho Mpunji alisema kuwa wameendesha semina hiyo ili kuwapa uelewa wadau wa mawasiliano wa Kanda hiyo ili wajue wajibu wao, majukumu ya mfuko na namna watakavyonufaika.

Alisisitiza kuwa mradi huo umeanzishwa ili kutatua changamoto za mawasiliano zinazoikabili jamii katika wilaya na mikoa mbalimbali hapa nchini ikiwemo kutoa ruzuku kwa ajili ya uwezeshaji vyombo hivyo.

Naye Ofisa Sheria wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Kanda ya Kati Joseph Kavishe aliwataka wadau wa mawasiliano kutumia mfuko huo ili kuboresha usikivu wa vyombo vyao vijijini.

Aidha aliwataka kufuata taratibu zote za uendeshaji vyombo vyao ikiwemo kulipa tozo ya asilimia 1 ya pato ghafi kwa mwaka kwa ajili ya kuchangia kwenye Mfuko wa Mawasiliano kwa wote ili kuendelea kunufaika na fursa zinazotolewa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles