CHRISTINA GAULUHANGA na TUNU NASSOR – DAR ES SALAAM
JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limesema uchunguzi wa tuhuma za kuwekewa sumu kwa Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Philip Mangula bado haujakamilika.
Akijibu swali kutoka kwa mmoja wa waandishi alipokuwa akizungumza nao jijini Dar es Salaam jana, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, alisema tukio hilo bado linafanyiwa uchunguzi ili kuwea kubaini undani wake.
“Bado tunaendelea na uchunguzi wa tukio la kulishwa sumu kwa Mangula na msitarajie kuwa kuna siku tutaeleza uchunguzi huo mbele yenu,” alisema Mambosasa.
Awali ilidaiwa kuwa Februari 28, mwaka huu, Mangula alidondoka ghafla katika ofisi ndogo za CCM Lumumba mara baada ya kumaliza kikao cha Kamati Kuu ya CCM kilichokuwa kikijadili masuala mbalimbali ambapo ilitoa adhabu kwa wanachama watatu waliokuwa na tuhuma za ukiukwaji wa maadili ndani ya chama hicho.
Katika kikao hicho, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe, alivuliwa uanachama kwa tuhuma za ukiukwaji wa maadili kwa mujibu wa katiba ya chama hicho na kanuni ya maadili na uongozi.
Machi 9, mwaka huu alipozungumza na waandishi, Mambosasa, alisema kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama, walibaini ndani ya mwili wa Mangula kulipatikana sumu.
Alisema kuwa jeshi hilo litachukua hatua kali kwa mtu yeyote atakayebainika kupanga, kuratibu au kusimamia utekelezaji wa uhalifu huo.