27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

TV3 kuwakutanisha Hamorapa, Patrick Kanumba katika shindano la nani Bingwa

Na Brighiter Masaki,Dar es Salaam

Kampuni ya StarTimes imewakutanisha Wasanii na Vijana wenye ushawahi kwenye mitandao ya kijamii katika shindano la Reality Show ya kutafuta mshindi walioipatia jina la ‘Bingwa’.

Akizungumza na Mtanzania Digital mara baada ya kutambulisha rasmi msimu wa kwanza wa show hiyo leo Jumanne Juni 29, 2021, Meneja Masoko wa Kampuni ya StarTimes, David Malisa, amesema ni wakati wa watazamaji kuona maisha halisi ya watu ambao wamekua wakijihusisha na vitu mbalimbali vya kiburudani kuanzia filamu, muziki, wajasiriamali pamoja na wanamitindo.

“Ni moja ya kipindi ambacho kitarushwa kupitia TV3 na washiriki wataanza kukaa kwenye jumba la kifahari Julai 12, mwaka huu huku sehemu kubwa ya washiriki ni vijana ambao wanaonekana katika jamii na kujihusisha na vingi hasa vya kiburudani.”

“Miongoni mwa wasanii walioshiriki ni msanii Harmorapa, Mwigizaji Patrick Kanumba na wengine wengi ambao tuliweza kuwapata kwa kupitia mchakato wa majina yao kupendekezwa kwenye ukurasa wetu wa Instagram,” amesema Malisa.

Aidha, Malisa ameeleza kuwa kupitia shoo hiyo, watazamaji wataweza kujishindia zawadi kwa Msimu wote wa shoo hiyo na watazamaji wataweza kuwapigia kura washiriki hao kwa kupitia StarTimes pamoja na mshindi kuibuka na zawadi ya gari ambalo bado halijafahamika pamoja na fedha Sh milioni 10.

“Watazamaji wataweza kushinda pia zawadi mbalimbali kupitia shoo hiyo, hivyo kwa sasa waendelee kuwapigia kura washiriki ili tuweze kupata washiriki 16 ambao wataingia kambini rasmi na kambi itachukua miezi miwili.

“Zawadi mbalimbali zitatolewa kwa washiriki wote huku mshindi ataibuka na gari ambalo tutatolea ufafanuzi siku za usoni lakini kwa sasa mshindi atapewa Sh milioni 10,” amesema Malisa.

Pia Malisa ameongeza kuwa shoo hiyo itaonyeshwa kuanzia Jumatatu hadi Jumamosi kuanzia saa 3 mpaka saa 4 kamili huku akiwasihi watazamaji kulipia visimbuzi vyao.

Kwa upande wake, Mzalishaji Mkuu wa shindano hilo, James Luvanda amesema vijana wengi wanatumia mitandao ya kijamii na wengi wamekuwa na ushawishi mkubwa sana katika jamii.

“Hivyo tumeona tuwakutanisha wale ambao wanafanya vizuri kwenye mitandao ya kijamii hasa Instagram na pia Facebook wanaweza kuitumia mitandao ya kijamii vizuri na wakaweza kubadilisha maisha yao ndio maana tumekuja na shoo ya Bingwa,” amesema Luvanda.

Kwa upande wake mmoja kati ya washiriki msanii wa filamu, Athuman Njaidi maarufu kama Patrick Kanumba, amesema kuwa wapo tayari kuingia kwenye mashindano japo ushindani ni mkubwa lakini anatarajia ushindi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles