27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

TUTACHUKUA VIWANDA VISIVYOENDELEZWA-DK. MERU

Na Mwandishi Wetu

-Dar es Salaam

SERIKALi imesema   uamuzi wa kuvichukua viwanda visivyoendelezwa ipo palepale hasa kwa wale walioshindwa   kutekeleza agizo la Rais Dk. John Magufuli.

Kauli hiyo ilitolewa   Dar es Salaam jana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji,  Dk. Adelhelm Meru, alipokuwa akijibu madai ya Chadema  wiki hii.

Chadema ilikosoa uamuzi huo wa Serikali kwa kuchukua viwanda hivyo.

Dk.  Meru aliwatahadharisha wawekezaji  waliobinafsishiwa viwanda ambao hawajaviendeleza na kuvifufua kwa mujibu wa mikataba, kutimiza wajibu wao.

“Hatua ya kuvirejesha viwanda hivyo serekalini limeanza kwa kasi. Baadhi ya wamiliki hawajafanya juhudi yoyote ya kuviendeleza na hivyo kuviacha viwe magofu au kutumika kwa matumizi yasiyo na tija na ambayo ni kinyume na mikataba waliyoisaini.

“Hali hii katu haiwezi kuendelea kufumbiwa macho,” alisema Dk. Meru

Alisema viwanda vilivyobinafsishwa zaidi ya miaka 20 iliyopita na ambavyo sasa ni mzigo kwa taifa, vilijengwa kwa fedha ya Watanzania.

Dk. Meru alisema wamiliki waliuziwa viwanda kwa mikataba ya kuviendeleza   vitoe ajira na kuingiza mapato serekalini lakini baadhi yao  wameivunja makusudi.

“Kwa sababu hiyo hatua ya kuvirejesha vile vilivyovunja mikataba halina ubaya wowote kama ilivyodaiwa na CHADEMA,” alisema.

Alitoa mfano  kwa viwanda vilivyotimiza wajibu ambavyo   ni pamoja na Kiwanda cha Bia (TBL), Kiwanda cha Sigara (TCC), viwanda vya saruji (Mbeya Cement, Tanga Cement, Twiga Cement).

“Viwanda  ambavyo Serikali inakusudia kuvirejesha serikalini ni vile  vilivyokiuka mikataba,” alisema.

Akijibu hoja ya Chadema kwamba hakuna viwanda vipya katika serikali ya awamu ya tano, Dk. Meru, alishangazwa na madai hayo kwa kusema kuwa kuna viwanda vilivyojengwa na vinavyoendelea kujengwa kwa mikopo ya taasisi za fedha za ndani.

Alivitaja viwanda hivyo kuwa ni Pipeline Industries, Global Packaging, Masasi Food Industries, CATA Mining Ltd.

Kadhalika amesema katika kipindi hiki   viwanda vilivyosajiliwa na kuanza utekelezaji kupitia TIC ni 224, kupitia EPZA ni 41 na kupitia BRELA ni 128 na  kwamba   viwanda vidogo na vya kati vilivyoanzisha na Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO) ni 2,243.

“Lengo la Serikali siyo kuvirejesha  viendeshwe na Serikali, bali kuvitangaza kwa wawekezaji wenye uwezo wa kuviendeleza waendeleze uzalishaji ambao utatoa fursa ya kuwapa watanzania ajira na kuingiza mapato serikalini,” alibainisha Dk. Meru.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles