24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

TUSICHUKULIE POA, DAWA ZA KULEVYA NI HATARI

KATIKA moja ya hotuba za Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, aliwahi kusema kuwa mtu akionja nyama ya mtu hawezi kuiacha. Kauli hii naweza kuifananisha na jinsi mtu akionja dawa za kulevya ilivyo vigumu kuyaacha.

Dawa za kulevya zimekuwa changamoto kubwa katika nchi mbalimbali duniani kwani vijana wengi wamepatwa na umauti kutokana na kuathiriwa na matumizi ya dawa hizo.

Licha ya Serikali kuwa na nia ya dhati ya kupambana na janga hili lakini mara kwa mara Taifa limekuwa likipoteza vijana wengi ambao ni nguvu kazi kutokana na matumizi ya dawa za kulevya.

Tumeshuhudia vijana ambao tayari walishaanza kupata mafanikio, lakini ndoto zao zimekuwa zikiishia pabaya hivyo kujikuta wakigeuka kuwa na maisha ya kuwa mateja na ombaomba barabarani.

Ipo mifano mingi ya watu ambao walikuwa wakiishi katika maisha mazuri lakini kutokana na kujiingiza kwenye utumiaji wa dawa za kulevya kuishia kuwa tegemezi na kuomba shilingi 100 au 200 babarani. Wenyewe wanasema kupinga mzinga!

Mfano ni kwa baadhi ya wasanii hapa nchini kama  Rehema Chalamila ‘Ray C’, Rashid Makwilo ‘Chid Benz,   Nando wa BBA na wengine wengi.

Wasanii hawa wamesemwa na kufuatiliwa zaidi kutokana na umaarufu wao lakini lipo kundi kubwa la vijana mtaani ambalo tayari limeteketea kwa madawa ya kulevya… kiukweli hawatamaniki hata kidogo.

Pita mitaa ya Manzese, Mwananyamala, Tandale, Ubongo, Magomeni na mingine ya jijini Dar es Salaam, utajionea jinsi gani nguvu kazi ya Taifa inavyozidi kupotea kwani huwezi kumaliza vichochoro viwili bila kukutana na kundi la vijana wakitumia mihadarati.

Kama wewe ni mtu wa kusafiri na daladala naamini utakuwa tayari umewaona vijana ambao wamedhoofika kwa madawa wakipiga debe barabarani ili hali wapate hata 200 ya kununulia madawa hayo ya kulevya.

Makundi mabaya na kutaka kuiga, ndiko kumelifikisha taifa katika hatua hii, kwani bila kujali vijana wamekuwa wakijiingiza kwenye makundi mabaya ambako wamekuwa wakiiga tabia tofauti na hata kujiingiza kwenye utumiaji wa madawa ya kulevya.

Imefikia hatua watu wanailahumu Serikali kwa kushindwa kupambana na uingizwaji na uuzwaji wa dawa hizo ambazo kwa kiasi kikubwa zimeathiri vijana wengi,  wakisahau kuwa kama vijana wangejitambua na kujua umuhimu wao katika ulimwengu huu hakuna mtu ambaye angemlalamikia mwenzake.

Hali ni mbaya, tutoe elimu kwa vijana wetu. Tuanzieni huku chini kabisa kwenye ngazi ya familia, tuwasaidie vijana. Dawa za kulevya siyo ujanja.

Hili ni tatizo serious. Kama mwananchi wa kawaida mwenye nia njema na nchi yako, anza kupiga vita dawa za kulevya kwa namna yoyote unayoweza kufanya.

Pongezi sana kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kwa kuanzisha harakati za kupambana na watumiaji na wauzaji wa dawa za kulevya kwa kasi.

Tumuunge Makonda kwa vitendo kwa kutoa elimu kwa vijana wetu. Tukiwaelimisha madhara yake, bila shaka hawatanunua. Maana yake ni kwamba, hata wauzaji wataacha maana hakutakuwa na watumiaji.

Mwisho, kwa vijana ambao bado hamjaanza hii kitu, aisee usidanganyike ukagusa. Ni hatari sana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles