25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Tundu Lissu afunguka Mwanza

Na BENJAMIN MASESE-MWANZA

MGOMBEA urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu  amesema amestushwa  na kupata wasiwasi juu ya  kitendo cha wakurugenzi watendaji wa halmashauri  nchi nzima kuitwa jijini Dodoma  na mgombea urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),Dk. John Magufuli.

Amesema  wakurugenzi watendaji wa halmashauri  kwa mujibu wa sheria ndio wasimamizi wa uchaguzi hivyo kitendo cha kuitwa  na Dk. Magufuli kimempa wasiwasi kwamba wanakwenda kupewa maelekezo ambayo yanaweza kufanana  na kuleta matokeo yaliyotokea  katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka 2019.

Akizungumza na wandishi wa habari jana katika ukumbi wa Nyakahoja unaomilikiwa na Kanisa Katoliki, Lissu  alimtahadhirisha Dk. Magufuli kwamba kama anataka kujiweka  katika mazingira magumu atoe maelekezo kwa wakurugenzi hao juu ya uchaguzi  wa mwaka huu huku akisisitiza kwamba ana asilimia 100 kupata kila  kitu  kitakachozungumzwa kikao hicho.

“Mwaka jana Dk. Magufuli aliwaita Ikulu watendaji wa kata na vijiji nchi nzima na akatoa maelekezo ambayo kila mtanzania anajua kilichotokea katika serikali za mitaa kwa wagombea wa vyama vya upinzani kuondolewa, siyo kwamba tumelisahahu hilo,  sasa  yeye atoe maelekezo na litalotokea litakuwa juu ya kichwa cha Magufuli.

“Kama anataka nchi hii ivuruguke achezee uchaguzi wa mwaka huu, kama anasema hataki kutembea kwenda mataifa makubwa basi ajue atatembezwa na sheria kwenda huko kujibu mashitaka, haiwezekani katikati ya kampeni anawaita wakurugenzi, yeye ni mgombea kwa nini akutane na wale ambao wana mamlaka ya usimamizi wa uchaguzi,”alihoji Lissu.

MABANGO-TRA

Akizungumzia juu ya  wagombea wa Chadema kutokuwa  na mabango mengi kama ilivyo kwa CCM, alisema walipewa masharti na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwamba wanapaswa kuyalipia na endapo watachapisha mabango yenye gharama ya Sh milioni 10 wanapaswa kulipia Sh milioni 20 kitendo ambacho hawakubaliani nacho kwa sababu siyo ya biashara.

Lissu alisema  licha ya kuwa na hali mbaya ya kiuchumi lakini Chadema inatarajia kupata fedhaa hivi karibuni ambapo wamejiandaa kutengeneza mabango makubwa ya wagombea akiwamo yeye na kuyabandika  nchi nzima huku akibainisha kwamba hawatayalipia TRA.

“Hatuna fedha ya kuchezea kwa sababu vyuma vimekaza kweli kweli, fedha iliyopo ndio inatusaidia katika kampeni lakini nasema wazi kwamba inawezekana tukapata fedha kwa awamu ya tatu ya kampeni zetu, tumejiandaa kutengeneza mabango makubwa na madogo ya kuyabandika  nchi nzima na hatutalipa hata senti moja TRA, nasema mabango hayo hayatabanduliwa na tusichezeana, kwanza nimepata taarifa CCM hawajalipia hayo mabango yao,”alisema.

ASIMULIA ALIVYOPIGWA  MAWE

Lissu alisema katika kampeni yake ya awamu ya pili amekumbana na matukio matatu kuanzia Mkoa wa Kigoma, Kagera na Geita ambayo hayakumfurahisha sana huku akilipongeza jeshi la polisi kwa kazi kubwa waliyofanya na kuimarisha usalama  wake kuanzia kwenye msafara barabarani  na mikutano yake.

Alisema akiwa mkoani Kagera walishambuliwa na mawe na wafuasi wa CCM waliokuwa juu ya ghorofa la ofisi ya chama hicho  wakati wanapita chini kitendo kilicholeta taharuki  licha ya polisi kudhibiti vurugu hizo  na kurejesha usalama.

“Tukio hilo limeleta doa katika kampeni hizo, na hii imetokana na CCM kuwa na hasira baada ya kuona watu wamejitokeza wengi ukizingatia alipopita Dk.Magufuli ilidaiwa walimzomea, tukio la pili nilipokuwa Geita Mjini  tulikuta vijana wakiwa na mabango wameziba barabara na walitaka kuleta fujo lakini tukawa wapole ndipo walipoanza tena kurusha mawe, bahati nzuri polisi waliweza kutumia mabomu ya machozi na kuwakamata baadhi.

“Walilinda mkutano wangu mpaka naondoka nipo salama, tukio la tatu ni ambalo hata mimi sikutegemea ni kupata watu wengi sana kuanzia Mkoa wa Kigoma, Kagera, Geita na Mwanza yaani mpaka nafarijika moyoni, ndio maana napata nguvu ya kufanya mikutano  kati ya 5 hadi 8 kwa siku ambapo kwa siku tatu ninakuwa na mikutano 20.

“Nilitaka kufanya mikutano hiyo kwa  helkopita lakini tumeambiwa rubani wetu ana zaidi ya miaka 55 hivyo ni mzee, kikubwa nashukuru watanzania hasa wa Kanda ya Ziwa kuniunga mkono,”alisema Tussu na kuendelea kulipongeza jeshi la polisi.

POLISI WAMENITENDEA HAKI

Kuhusu jeshi la polisi, alisema vimemtendea haki katika kampeni hasa awamu ya pili, jambo ambalo hakulirajia kabisa huku akidai kuwa anasikitishwa na kitendo cha baadhi ya polisi kuhamishwa na kushushwa vyeo kutokana na kuimarisha usalama wake.

“Jeshi la polisi limebadilika sana na wamenipa ushirikiano wa hali ya juu kuanzia msafara na mikutano yangu, mtu kama mimi ambaye ni muathirika wa matukio ya polisi nimeshtushwa lakini maeneo ambayo nilipewa ushirikiano na polisi nimeambiwa wameondolewa  na kuhamishwa, nimedokezwa kule Songwe, Geita, Kagera  na Kigoma wamekumbana na hali hiyo, binafsi hadi sasa siwezi kuwasingizia jambo kwa namna walivyonilinda,”alisema.

MIKOPO

Kuhusu mikopo ya elimu ya juu, alisema endapo atafanikiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atahakikisha  anarejesha asilimia tatu ya mkopo kama ilivyokuwa awali wakati bodi ya mikopo inaanzishwa.

Alisema watu wasio na nia njema  na Watanzania wameamua kupandisha asilimia ya mkopo kutoka tatu hadi 14 jambo ambalo linaleta ugumu wa kurejesha.

Pia alisema atahakikisha anaondoa ubaguzi uliopo sasa kati ya waliosoma binafsi na umma.

KUHUSU KUTUMWA NA MABEBERU

Hata hivyo alisisitiza kwamba  kuna watu wachache wanasema  ametumwa na mabeberu kugombea urais ambapo alifafanua kwamba Tanzania bila kushirikiana na mataifa yaliyoendelea haiwezi kupata maendeleo.

Alisema hao wanaoitwa mabeberu endapo wataamua kutoshirikiana na Tanzania ndani ya  wiki moja watapata shida sana na kuwataka watanzania kuachana na propaganda hizo kwani miradi mikubwa nchini inafadhiliwa na mataifa makubwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles