25.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

TUNAWATAKIA WATANZANIA WOTE KRISMASI NJEMA KESHO

Decoration Christmas Tree Decorations Ideas 2014 Christmas Tree

KESHO Wakristo wa Tanzania wanaungana na Wakrito wengine kote duniani kusherehekea Sikukuu ya Krismasi.

Viongozi wa familia za Kikristo watawaongoza na kuwahimiza wanafamilia nchini kote kwenda kuhudhuria ibada makanisani.

Kwa vyovyote vile ibada hizo zitakwenda sambamba na mahubiri mbalimbali kutoka kwa viongozi wa Kikristo ambao watazungumzia kuzaliwa kwa Yesu Kristo, mema aliyoyahubiri na masuala mbalimbali yanayoisibu nchi yetu kwa sasa.

Tunasema kwa furaha kubwa kabisa  kuwa tunawatakia Wakristo wote wa Tanzania na ulimwengu kwa ujumla wao Krismasi njema kesho.

Aidha, Watanzania ambao si Wakristo tunawasihi wawape ushirikiano katika kila hatua ya sherehe hizo kwa upendo mkubwa unaoashiria undugu.

Kama inavyofahamika, Krisimasi ni siku ya kukumbuka kuzaliwa kwa Yesu Kristu zaidi ya miaka 2000 iliyopita.

Kwa Mkristo atakayebahatika kuiona siku ya kesho, kwake ni siku ya furaha kubwa, ni siku ya ibada na kuadhimisha kuzaliwa kwa mwana wa Mungu. Pia ni siku ya kula na kunywa kwa kadiri mtu awezavyo na kwa kadiri atakavyojaliwa na Mungu.

Hii ina maana kuwa ni kula vyakula na kunywa vinywaji kwa kiwango kinachokubalika bila kupitiliza ili asilete usumbufu kwa watu wengine.

Siku ya Krismasi ni fursa ya toba na ya kusherehekea kwa kauli njema na kukumbushana kuendeleza mema siku zote katika jamii.

Haitarajiwi kwa namna yoyote kusikia mahali na eneo lolote la nchi hii, na dunia kwa ujumla wake, taarifa yoyote mbaya inayomchukiza Mungu kufanywa na Mkristo au mtu mwingine yeyote kwa kisingizio cha furaha iliyopitiliza au ulaji na unywaji uliokithiri.

Tunawakumbusha Wakristo wote kuwa sherehe hizi ziendane na kutoa misaada kwa yatima, wajane, wagonjwa, masikini na wengine wote wenye kuhitaji.

Vilevile siku ya kesho iwe siku ya kudhihirisha mshikamano wa kitaifa kwa kuonyesha ushirikiano na madhehebu mengine kwa sababu binadamu wote ni wana wa Mungu mmoja.

Kwa hiyo wakati wakisherehekea, ni muhimu kwa Wakristo wote nchini kuyakumbuka yote haya ili sherehe za kusindikiza siku hii ziwe chagizo ya upendo, mshikamano, undugu na umoja wa kitaifa.

Tunapenda kusisitiza kuwa Watanzania ambao si Wakristo wawape ushirikiano katika kila hatua ya sherehe hizo kwa upendo mkubwa unaoashiria undugu.

Tunasema hivi kwa sababu watu hawa wanapaswa kudhihirisha mshikamano wa kitaifa kwa kuonyesha ushirikiano na madhehebu mengine kwa kuwa wote ni wana wa Mungu mmoja.

Hii itadhihirisha kuwa nchi yetu haina dini ila watu wake ndio wenye dini na imani zinazotofautiana. Kwamba tuna nchi moja yenye upendo na mshikamano.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa New Habari (2006) Ltd, Mhariri Mtendaji Mkuu, wahariri wote na wafanyakazi wa New Habari (2006) Ltd katika ujumla wao wanachukua fursa hii kuwatakia Wakristo wote siku ya Krismasi njema na yenye baraka tele.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles