24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Tumuenzi Nyerere kwa kurudi mstarini

Hayati Mwalimu Julius K. Nyerere
Hayati Mwalimu Julius K. Nyerere

TANZANIA  ya leo inaweza kuelezwa kuwa ilikuwa imeshachepuka na kuondoka katika mstari uliokuwa umedhamiriwa na waasisi wake na hususani Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambaye Oktoba 14, itatimia miaka 17 tangu afariki.

Ni sahihi  kusema kuwa  kimwili hayupo nasi lakini maneno na kauli zake pamoja na mafundisho yake bado yanaishi  kutokana na sababu moja kuu kwamba kauli na mafundisho yake  hayo yalikuwa ni mwanga  na dira  ambayo Tanzania inatakiwa kuifuata.

Lakini katika miaka ya hivi karibuni  wale waliopewa dhamana ya kuiongoza nchi  wameonekana  kushindwa kufuata  mafundisho  aliyokuwa akiyatoa Mwalimu.

Hilo linadhihirishwa kwa mambo ambayo yameibuliwa na Awamu ya Tano  inayoongozwa na Rais John Pombe Magufuli. Mojawapo ni suala la kodi ambapo katika mafunzo ya Mwalimu alisema, “Nazungumza habari za kutokusanya kodi. Kutokusanya kodi ni sifa moja ya viserikali corrupt popote pale. Popote, wala usifikiri ni Tanzania peke yake…Serikali corrupt popote pale, haitozi kodi.

“Serikali corrupt inatumwa na wenye mali. Inawafanyia kazi wenye mali. Serikali corrupt itamwambieje mwenye mali, kwamba ‘utalipa, usipolipa utakiona!’ Atacheka tu huyu. Atakwambia ‘unaniambia hivyo wewe? kesho siji basi!

Wakati Serikali ilipoanza kukusanya kodi kutoka kwa wafanyabiashara na hususani waliokuwa wanapitisha bidhaa zao katika Bandari ya Dar es Salaam  na ambao walikuwa hawalipii kodi bidhaa zao  hapo ndipo ilionyesha ni kwa jinsi tulivyokuwa tumekengeuka.

Ilikuwa ni dhahiri kuwa Tanzania hii ilikuwa imechepuka na kuondoka katika mstari kwa kulipuuza somo  kuhusu kodi alikuwa amelitoa Mwalimu Nyerere.

Hatua hiyo inaonesha kuwa kutolipwa kwa kodi kulitokana na kuchepuka katika mkondo wa kudai kodi  na kuingia katika mkondo usio mnyoofu wa kula rushwa na hivyo kuikosesha jamii (Serikali) haki  yake ya kupata nyenzo ya kupeleka maendeleo ya wananchi.

Katika mchepuko hatari ni ule wa kutotambua vyeo ni dhamana na vitumike kwa faida ya wote  lakini vikawa ndio nyanzo vya kuvuna jasho la mvuja jasho kwani badala ya kuwajibika kwa ajili ya umma  ikawa ni kuwajibika kwa ajili yao na wana wao.

Katika mtazamo wa kauli za Mwalimu aliona kuwa baadhi ya viongozi walikuwa wameshapandikiza mazingira ya kupuuza  hisia za utaifa za uzalendo, ujasiri, kujituma, kuwajibika na kwamba walikuwa wamejibadili kitaswira kama watu wanaohama kesho na hivyo kuwa na haja ya kukusanya  kila walichokiona ili wakafaidi mbele ya safari.

Taswira hiyo ilionesha kuwa  wao ndio waliokuwa na meno  na wanajua kutafuna  ndio maana leo hii linapotajwa  suala kuwa  walikuwapo wafanyakazi hewa ndani ya taasisi za umma  na kwamba hata marehemu walikuwa wakilipwa malipo hiyo inakuwa ni fedheha ambayo Mwalimu hakuwa ameisahau katika masomo yake.

Wakati Serikali ya Awamu ya Tano ikiwabaini kuwapo kwa kadhia ya mambo hewa kuanzia wafanyakazi hewa, malipo hewa  na hata wanafunzi hewa ni dhihirisho kwamba mchepuko uliokuwa umefanyika katika  enzi za  uongozi wa mazoea  ulikuwa ni wa kujenga kada ya wavuna jasho wachache walioifurahia keki ya Taifa na wavuja jasho wakiambulia makombo au wakiendelea kusinyaa.

Katika kuchepuka  huko  ambako nchi iliingia  ni dhahiri waliokuwa na dhamana  walikuwa wakihanikiza uendelevu wa kuvuna jasho na kuwaacha wavuja jasho wakiwa hoi  ndani ya umaskini, ujinga na maradhi na wakishamirisha dhuluma. Hili Mwalimu alilionyea katika masomo yake.

Wavuna  jasho waliiweka kando kanuni njema katika masomo hayo ya kushirikiana na jamii kwa ujumla  kuijenga nchi, badala yake  wakaunda mtandao wao wa kushirikiana kuitafuna nchi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles