30.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

‘Tumbaku chanzo cha saratani duniani’

tumbakuVeronica Romwald na Esther Mnyika, Dar es Salaam

SERIKALI imeombwa kudhibiti uingizwaji na utengenezaji wa bidhaa za tumbaku nchini kwa sababu utafiti unaonyesha asilimia 32 ya saratani zote zinasababishwa na zao hilo.

Pia imetakiwa kuchukua hatua kali ya kudhibiti kasi ya ongezeko la vijana wanaovuta bidhaa hizo, wakichochewa zaidi na uingizwaji wa tumbaku aina ya shisha na sigara za umeme.

Rai hiyo ilitolewa jijini Dar es Salaam jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Kudhibiti Matumizi ya Tumbaku Tanzania (TTCF), Lutgard Kagaruki, wakati alipokuwa akitoa mada kwenye semina ya siku moja ya waandishi wa habari, iliyolenga kuwajengea uelewa juu ya namna tumbaku inavyochangia ongezeko la ugonjwa huo.

“Tumbaku huua wavutaji milioni sita kwa mwaka duniani, huku wengine 600,000 wasiovuta wakivutishwa moshi wa tumbaku,” alisema.

Alisema tumbaku inachangia kwa kiasi kikubwa matatizo ya upungufu wa nguvu za kiume, huku Serikali ikitumia kiasi kikubwa cha fedha takribani dola za Marekani milioni 4 kwa mwaka kugharamia matibabu.

“Hii ni kwa mujibu wa utafiti tulioufanya katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI) na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) mwaka 2009 na hapo hatukwenda maeneo ya vijijini, hivyo huenda hali ikawa mbaya zaidi,” alisema.

Alisema ni vyema Serikali ikatunga sheria kwa ajili ya kusimamia udhibiti wa bidhaa hiyo kama ambavyo ilikubali mkataba wa kimataifa wa kudhibiti matumizi ya tumbaku.

“Tanzania iliridhia mkataba tangu 2007. Haina budi kutekeleza kikamilifu kwa kutunga sheria madhubuti ya kudhibiti matumizi ya tumbaku inayoendana na matakwa ya mkataba wenyewe,” alisema.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa ORCI, Dk. Julius Mwaiselage, alisema idadi ya wagonjwa imekuwa ikiongezeka ambapo hadi sasa imefikia asilimia 100.

“Takwimu zetu zinaonyesha mwaka 2000 hadi 2005 tulikuwa tunapokea wagonjwa wapya 2,400 hadi 2,500 kwa mwaka, idadi imeongezeka hadi kufikia wagonjwa wapya 5,500 mwaka 2015,” alisema.

Alisema hali hiyo inachangiwa zaidi na mfumo wa maisha ya sasa ambapo watu wengi wamekuwa hawazingatii ulaji bora, matumizi ya pombe, uvutaji wa sigara, kutokufanya mazoezi na mambo mengineyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles