27 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Tuendelee kuishinikiza Serikali kuhusu mabadiliko sheria ya habari- Wanahabari

Na Faraja Masinde, Mtanzania Digital

Wadau wa Tasnia ya Habari nchini wamesema kuwa mabadiliko ya Sheria ya Habari ni muhimu katika kuvirejeshea nguvu vyombo hivyo.

Hivyo wamehimiza kuendelea kuishinikiza serikali juu ya mabadiliko hayo.

Wakizungumza na Mtanzania Digital kwa nyakati tofauti baadhi ya waaandishi wa habari wamesema kuwa serikali inapaswa kuharakisha mchakato huo wa mabadiliko ya sheria ili kuleta ufanisi ambao umepungua katika vyombo vingi.

Akizungumzia kuhusu uratibu wa matangazo mmoja wa wanahabari hao ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini amesema kuwa suala hilo kubaki mikononi mwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo ni kuvinying’onyesha vyombo hivyo hatua ambayo imeua uchumi wa vyombo vingi.

“Ukiangalia suala hili la uratibu wa matangazo ya taasisi zote za Serikali yanayopelekwa katika vyombo vya habari kuwa chini ya Mkurugenzi wa Idara ya Habari, ni bayana kwamba mpango huu ulikuwa na nia ya kuua uchumi wa vyombo vya habari ambavyo pengine vingeonekana kuikosoa serikali au kutokufanya vile ambavyo inataka.

“Kwa maana hiyo suala hili likiwa chini ya mtu mmoja anakuwa na uwezo wa kuamua kwamba chombo flani kisipewe matangazo na ndiyo maana utaona katika awamu iliyopita vyombo vingi vilishindwa kujiendesha na hatimaye kufungwa mfano gazeti la Mtanzania na mengine,” amesema mmoja wa wanahabari hao ambaye hakutana kutajwa jina.

Upande wake Hassan Daudi akizungumzia changamoto hizo za sheria amesema kwamba wanahabari wanakila sababu ya kuendelea kuishinikiza serikali katika kuhakikisha kuwa mabadiliko hayo yanafanyika.

“Mimi kama mwandishi wa habari naungana na wanatasnia wenzangu kwani nami ni mwathirika wa sheria hizi ambazo tunafanya juhudi zibadilishwe, kwani sehemu kubwa ya sheria zilizopitishwa hasa awamu ya tano ililenga kubana uhuru wa vyombo vya habari ikilinganishwa na awamu ya nne ambapo vilikuwa na uhuru wa kufanya kazi vizuri na kuibua changamoto mbalimbali zikiwamo kashfa za Escrow ambapo kwa kiasi kikubwa vilisaidia serikali na wananchi.

“Lakini baadaye tukaona mabadiliko ya haraka ya sheria katika awamu ya tano, ukiangalia kipindi hicho uhuru huo haukuwepo kwani vyombo vingi vilibanwa na sheria na hivyo kukosa nguvu ya kuikosoa serikali.

“Kwa hiyo tumeshuhudia mijadala ikiendelea baina ya serikali na wadau wa habari hivyo natumaini kuwa itazaa matunda mazuri kwani pia tumemsikia Waziri Nape ameahidi kuwa yale yaliyojadiliwa na kuwasilishwa na wadau yanafanyiwa kazi na kwa kiasi kikubwa yatachukuliwa, kwa hiyo tunasubiri tuone mswada utakaopelekwa bungeni kwa ajili ya marekebisho ya hizi sheria utakuwaje ili tuone nia njema ya serikali, muhimu ni kuendelea kuishinikiza ili kuhakikisha kuwa mabadiliko haya yanafanyika,” amesema Daudi.

Akizungumza hivi karibuni Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania(TEF), Deodatus Balile amesema kuwa wadau wa habari nchini wanasubiri matokea ya vikao vya serikali na wanahabari kuhusu mabadiliko sheria ya habari nchini nakwamba mchakato huo umefikia pazuri.

‘‘Kwa hakika sisi kama wadau wa habari tumefika hatua nzuri na hata kuwa na matumaini chanya baada ya kikao cha mwisho kati ya wanahabari na serikali. ‘Wakati unaofuata ni wa serikali na hatua zake katika kuelekea mabadiliko sheria ya habari, lakini mpaka hapa tulipofika, tunaamini kuna jambo linakwenda kutokea,’’ amesema Balile.

Aliongeza kuwa jambo linalofurahisha zaidi ni ushirikishwaji wa taasisi zote za habari nchini katika mchakato wa mabadiliko ya sheria ya habari.

‘‘Kwa kuwa wadau wa habari tunapigania kitu kimoja, tuliamua kwa pamoja kujiweka chini ya mwavuli tunaouita CoRI (Wadau wa Kupata Habari).

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles