27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

Trump apoteza trilioni 1.7/- kipindi cha mwaka mmoja

MGOMBEA urais wa Marekani kupitia Chama cha Republican nchini Marekani, Donald Trump
MGOMBEA urais wa Marekani kupitia Chama cha Republican nchini Marekani, Donald Trump

NEW YORK, MAREKANI

MGOMBEA urais wa Marekani kupitia Chama cha Republican, Donald Trump, amepoteza dola milioni 800 sawa na Sh milioni 1.7 ya utajiri wake katika kipindi cha mwaka mmoja, kwa mujibu wa Jarida la Forbes.

Jarida hilo linasema kwa sasa utajiri wa bilionea huyo wa New York ni dola bilioni 3.7.

Forbes wanasema kushuka huko kwa thamani ya utajiri wake kunatokana na kudorora  kwa biashara ya nyumba na ardhi katika soko la New York.

Trump aliyewahi kuandika kitabu kiitwacho Midas Touch, yaani Mguso wa Midas, aliyeaminika kubadilisha kila alichogusa kuwa dhahabu, amekuwa akisema kuwa Rais wa Marekani kwa sasa anaweza kuwa mtu mwenye busara katika biashara na majadiliano.

Wakati wa mdahalo wa urais Jumatatu wiki hii, alijigamba na kusema: “Nina mapato makubwa, wakati umefika kwa taifa hili kuwa na mtu anayefahamu mengi kuhusu fedha.”

Hata hivyo, mpinzani wake katika kinyang’anyiro hicho kutoka Chama cha Democratic, Hillary Clinton, alimponda akisema utajiri wake umetokana na urithi na mkopo kutoka kwa baba yake.

Aidha, makadirio ya Forbes na Jarida jingine ya Fortune na Bloomberg yanauweka utajiri wake kati ya dola bilioni 3 na 3.9, ikiwa ni kinyume na anavyosema kuwa ana dola bilioni 10.

Forbes ambao wamekuwa wakikadiria utajiri wa Trump kwa zaidi ya miongo mitatu, wanasema kushuka kwa utajiri wake kumetokana na kudorora kwa soko la nyumba, ofisi na ardhi mjini New York.

Kati ya majumba 28 ambayo yalichunguzwa na Forbes, 18 yalishuka thamani, likiwemo jumba maarufu la Trump Tower lililopo Manhattan.

Jumba lake lililopo 40 Wall Street na klabu yake ya Mar-a-Lago iliyopo Palm Beach, Florida, pia vilipoteza thamani, kwa mujibu wa Forbes.

Lakini majumba saba ya Trump, likiwemo la pili kwa urefu mjini San Francisco, yalipanda thamani.

Na inakadiriwa amewekeza dola milioni 50, zikiwa ni fedha zake binafsi kwenye kampeni kufikia sasa.

Aidha, Forbes wanakadiria kuwa matamshi yake dhidi ya wahamiaji wa Mexico yalimgharimu dola milioni 100 kupitia mikataba aliyopoteza kwenye mashirika makubwa kama vile NBC Universal, Univision na Macy’s.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles