23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Trump apitishwa kuwania urais Marekani

Donald Trump
Donald Trump

CLEVELAND, MAREKANI

MKUTANO Mkuu wa Chama cha Republican umempitisha kwa kishindo bilionea Donald Trump kuwa mgombea wake katika uchaguzi wa urais wa Marekani utakaofanyika Novemba mwaka huu.

Mara tu baada ya Trump kupitishwa viongozi wa Baraza la Wawakilishi wa chama hicho walijikuta wakitumia muda mwingi kutafuta namna ya kukijenga upya chama hicho.

Aidha walitumia muda mwingi kumshambulia mgombea urais wa Chama cha Democrat, Hillary Clinton, kuliko muda waliotumia kumuelezea mgombea wao.

Spika wa Baraza la Wawakilishi, ambaye ndiye aliyelitambulisha rasmi jina la Trump kwenye mkutano huo mjini hapa, Paul Ryan, amewataka wajumbe wote kuungana pamoja, baada ya mgawanyiko mkubwa ndani ya chama dhidi ya Trump.

“Sasa mnasemaje? Mnasemaje kuhusu kukiunganisha chama hiki katika wakati huu muhimu ambao umoja ndio kila kitu. Tuelekeze mapambano yetu sasa dhidi ya wapinzani wetu tukiwa na mawazo bora zaidi. Tukashambulie na tubakie kwenye eneo la mashambulizi,” alisema Ryan.

Kampeni za kutaka Republican isimchague Trump zilishindwa kwenye hatua zake za awali.

Maandamano ya kumpinga nje ya jengo la mkutano na majibizano kati ya wanaomuunga mkono na wapinzani yalizimika mara tu baada ya kutangazwa rasmi, huku wajumbe waliomkataa wakitoka ukumbini.

Mwenyewe Trump aliwaambia maelfu ya wajumbe wa chama chake kwamba ana hakika atashinda kwenye uchaguzi wa urais, huku akisema anaona fahari kuwa mteule wao.

Aliwashukuru watoto wake kwa kumuunga mkono tangu hatua za awali, na kumsifu mgombea wake mwenza, Gavana Mark Pence wa Indiana, huku akiendeleza kaulimbiu yake ya kuirejeshea Marekani hadhi yake ya zamani.

“Huu utakuwa uongozi, ambao unawaweka watu wa Marekani kwenye nafasi ya kwanza. Tutazirejesha ajira zetu, tutalijenga upya jeshi letu lililoporomoshwa na kuwahudumia wanajeshi wetu wa zamani, tutakuwa na mipaka imara, tuliangamiza kundi la Dola la Kiislamu, tutarejesha utawala wa sheria.”

Hadi kufikia hatua hii, bilionea huyo ambaye hana uzoefu wowote wa kisiasa, alishawaangusha waliokuwa wapinzani wake 16 kuwania tiketi hiyo, wakiwamo magavana na maseneta waliokuwa na uzoefu mkubwa ndani ya Republican.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles