25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Trump agoma kuwalazimisha Wamerakani kuvaa barakoa

WASHINGTON, MAREKANI

RAIS wa Marekani, Donald Trump ameapa kutolazimisha Wamarekani kuvaa barakoa kama njia moja ya kudhibiti usambaaji wa virusi vya corona.

Maoni yake yanawadia wakati daktari mkuu nchini humo wa magonjwa ya kuambukiza, Dk. Anthony Fauci, amesisitizia viongozi wa majimbo na maeneo kulazimisha raia kuvaa barakoa.

Dk. Fauci ameongeza, ni muhimu sana na kila mmoja anastahili kuzitumia kila wakati.

Nchini Marekani kuvaa barakoa kumegeuka kuwa suala la kisiasa zaidi.

Magavana wengi wa majimbo, sasa wametoa agizo kwamba ni lazima kuvaa barakoa mtu anapotoka nje, wala sio hiari tena.

Miongoni mwao ni magavana wa Republican akiwemo Kay Ivey wa Alabama, ambaye amebadili msimamo wake wa awali na sasa amesema kuwa ni lazima kila mmoja kuvaa barakoa.

Rais Trump ambaye awali alikuwa anapinga uvaaji wa barakoa hata kwake binafsi, alivaa barakoa hadharani kwa mara ya kwanza Jumamosi iliyopita.

Akizungumza na kituo cha habari cha Fox News Ijumaa, Trump alisema hakubaliani kulazimisha watu kuvaa barakoa akidai kuwa raia kwa kiwango fulani wanastahili kuwa na uhuru.

Mapema wiki hii, Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa Marekani (CDC), kilitoa taarifa na kuasa kila mmoja kuvaa barakoa.

“Sio kwamba tumeshindwa kabisa katika vita dhidi ya COVID-19,” Mkurugenzi wa CDC Dk. Robert R Redfield alisema. 

“Kujifunika nyuso ni moja ya silaha muhimu ya kupunguza na kusitisha usambaaji wa virusi, – hasa kila mmoja anapovaa katika ya jamii.”

Katika jimbo la Kusini la Georgia, Gavana wa Republican, Brian Kemp amesisitizia raia kuvaa barakoa kufikia mwezi ujao.

Kemp alitoa ombo hilo kwa wakaazi licha ya kuchukua hatua ya kisheria siku moja kabla dhidi ya Meya wa Atlanta, Keisha Lance Bottoms, kufanya  uvaaji wa barakoa kuwa lazima kwenye mji huo.

Bottoms yeye binafsi amepatikana na virusi vya corona.

Maofisa wa mji wa Oklahoma pia nao wanafikiria kufanya uvaaji wa barakoa kuwa lazima ikiwa jimbo halitachukua hatua.

Majimbo kadhaa Marekani yameathirika hasa ya kusini yanashuhudia ongezeko la juu la maambukizi yaliyothibitishwa ya virusi vya corona.

Mamia ya wahudumu wa afya wanajeshi wamepelekwa Texas na California kusaidia maofisa kukabiliana na maambukizi mapya ya virusi vya corona na Texas na Arizona, malori yenye majokofu yametumwa kuhifadhi miili ya waliokufa.

Katika wiki za hivi karibuni, hospitali zimeshuhudia wagonjwa wengi kupita kiasi, Florida pia imetoa taarifa kuwa vyumba vya wagonjwa mahututi vimejaa na hawawezi tena kukubali kupokea wagonjwa zaidi.

Dk. Anthony Fauci amesema kuvaa barakoa ni muhimu.

Katika baadhi ya miji na majimbo, yana wakati mgumu kukabiliana na ongezeko kubwa la wanaohitajika kupimwa virusi vya corona.

Huko Pittsburgh, Pennsylvania, watu wanaoshukiwa kupata maambukizi wameombwa kujitenga majumbani mwao kwa siku 14 badala ya kwenda kwenye vituo vilivyotengwa kupimwa, huku Hawaii bado inaendelea na kanuni yake ya kuweka wageni wote karantini kwa mwezi mmoja zaidi, kwasababu ya upungufu wa vifaa vya kupimia.

SHULE

Mamilioni ya watoto ikiwemo katika majimbo mawili maarufu ya Texas na California, wamearifiwa kwamba shule hazitafunguliwa kwa mwaka mpya wa masomo.

Elimu na suala la lini shule zinafunguliwa pia limegeuzwa kuwa la kisiasa.

Mwongozo mpya wa kufunguliwa kwa shule ulitarajiwa kutolewa wiki hii lakini vyombo vya habari vya Marekani vimeripoti kwamba umechelewa.

Marekani bado imesalia kuwa nchi yenye maambukizi ya juu ya virusi vya corona duniani.

Sasa hivi nchi hiyo imethibitisha maambukizi ya virusi vya corona milioni 3.6 na vifo zaidi ya 139,000 –ikiwa ni idadi kubwa zaidi duniani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles