25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Trafiki watatu wafukuzwa kazi

traffic mapenziNA RENATHA KIPAKA, BUKOBA

JESHI la Polisi mkoani Kagera limewafukuza kazi askari wake watatu kwa kulifedhehesha jeshi hilo kutokana na kitendo cha kupiga picha inayowaonyesha wawili kati yao wakinyonyana ndimi wakiwa kazini.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Henry Mwaibambe, alisema kitendo kilichofanywa na askari hao kimeshusha hadhi ya jeshi.

Aliwataja askari hao waliofukuzwa ni F.7788 PC Mpaji Mwasumbi, G 2122 PC Fadhili Linga na WP.8898 Veronica Mdeme ambao wote ni wa Kikosi cha Usalama Barabarani Wilaya ya Misenyi.

Alisema PC Mpaji na WP Veronica walipiga picha inayokwenda kinyume na maadili ya Jeshi la Polisi wakiwa kazini, huku PC Fadhili akiingia matatani kwa kuwapiga picha hiyo chafu askari wenzake na kuisambaza kwenye mitandao ya kijamii.

Kamanda Mwaibambe alisema picha hiyo ilianza kuonekana katika mitandao mbalimbali ya kijamii mapema wiki hii.

Alisema askari PC Fadhili alipiga picha hiyo mwaka 2012 kwa kutumia simu yake ya kiganjani na kuitunza, lakini wiki hii aliamua kuisambaza kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii kitendo ambacho ni kinyume na kazi yake.

“Napenda kuthibitisha kuwa picha hii iliyoonekana kwenye mitandao ya kijamii ni picha halisi ambayo haijachakachuliwa kabisa.

“Maadili ya kijeshi yapo kisheria na askari wetu wanafundishwa namna ya kuishi katika maisha ya utumishi wa jeshi na si vinginevyo.

“Jeshi halikubaliani na vitendo hivi, ikitokea askari kwenda kinyume lazima achukuliwe hatua kali,” alisema Kamanda Mwaibambe.

Taarifa zaidi kutoka mkoani Kagera, zinaeleza baada ya kusambazwa kwa picha hiyo na kuonekana katika mitandao ya kijamii, WP Veronica alianguka ghafla na kupoteza fahamu kwa mshtuko wa tukio hilo.

Kutokana na hali hiyo, majirani waliokuwa karibu na nyumbani kwake walilazimika kumpatia msaada na kumkimbiza hospitali kwa matibabu, ambako aliruhusiwa juzi jioni kabla ya kutiwa mbaroni.

DAR ES SALAAM

Wakati hayo yakiendelea, Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, limewahamisha askari wake, WP 5863 Quine na WP 3548 Koplo Maeda kutoka Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Ilala kwa kukiuka maadili ya kazi.

Taarifa ya ndani ya Oktoba 2, mwaka huu ya Kikosi cha Usalama Barabarani Makao Makuu Dar es Salaam iliyosambazwa kwenye mitandao ya kijamii, imesema askari hao walisimamisha gari dogo na baada ya dereva kujitetea, waliendelea kutafuta makosa hali iliyosababisha abiria aliyekuwa mgonjwa kufariki.

Kutokana na tukio hilo, makamanda wa polisi wa wilaya zote za Mkoa wa Kipolisi wa Dar es Salaam wametakiwa kuwakumbusha askari wao kuepuka kutolazimisha kutafuta makosa ambayo hayana madhara.

“Makosa ambayo hayana madhara katika kusababisha ajali mfano ni vifaa vya kuzimia moto, rangi, kadi kutoandika anuani, motor vehicle, leseni chini ya siku 30 na kadhalika,” lilisomeka agizo hilo kwa makamanda hao wa polisi.

- Advertisement -

Related Articles

6 COMMENTS

  1. Wamefukuzwa kazi kwa sababu picha zao zimeonekana katika mitandao hivyo hawana maadili. Maadili ya kuwajibisha katika nchi yetu sasa yanawalenga wafanyakazi wa vyeo vya chini si kwa vyeo vya juu. Mfano, tukio la Profesa Kapuya na mwanafunzi wake kama lilivyoripotiwa kwa kina na gazeti la Tanzania Daima likiwa limeshsheni ushahidi wa kutosha sikuona polisi wakichukua hatua japokuwa taarifa walipewa. Hii maana yake katika nchi yetu kuna mtindo wa kuhukumiana kwa mtindo wa matabaka. Kwa mtindo huu tuendako si salama.

    • Professor kapuya na huyo mwanafunzi,Je ni waajiliwa wa jeshi la polisi?Tambua ya kwamba,kila wizara au taasisi au idara inayomilikiwa na serikali ina maadili yake ya kazi kwa muujibu wa sheria.Hivyo polisi hawapo kisheria kwa kazi ya kuwafukuzisha watu kazi ambao hawapo kwenye wizara yao au idara yao.TAFAKARI HILI!

  2. Kitu kikubwa kilichopewa uzito na viongozi wa polisi juu ya kuwachukulia hatua askari hawa ni KUKOSA MAADILI jambo ambalo halikupewa uzito unaostahiki na bunge la katiba kiasi cha kuliodoa neno hili katika orodha ya tunu za Taifa kama lilivyopendekezwa na kamati ya muheshimiwa Warioba.MAADILI NI KIGEZO KIKUBWA SANA kwa watumishi wa ngazi zote . Lakini wale wasiojali tumewaona jinsi walivoendesha bunge la katiba

  3. Mtu akifanya kosa inatakiwe aadhibiwe, sawa. Kosa lazima kupimwa katika mizani. Kosa la mkuu wa polisi Mkoa wa Iringa na polisi wenzake waliohusika katika kumwua mwandishi Mwangosi, Mkuu wa posili alibembelezwa na waandishi aingilie kati, kusudi Mwangosi asiuawe, naye akashusha kio na kupandisha. Hicho ni kitendo cha kuua mwandishi asiye na kosa. Alipandishwa cheo, na kwenda makao makuu. Hao mapolisi watatu wamefukuzwa kazi kwa la nidhamu. Kuua na nidhamu, kuua ni kosa zito, kwa wenzetu walioendelea, waziri, mkuu wa polisi na wote waliohusika ilitakiwa wafukuzwe na kufungwa hasa yule mkuu wa polisi wa mkoa. Uzito wa kosa la watatu ni mdogo wangepata viboko viwili viwili basi.

  4. Adhabu ya Dar Es Salaam ya kuwahamisha askari “waliosababisha” kifo cha mgonjwa ndani ya garihaikupaswa kutolewa kabla ya daktari kuchunguza na kutoa taarifa kama huyo mgonjwa alifariki kwa sababu ya kucheleweshwa hospitaliau la. Na kama jibu lingekuwa hilo basi askari hawa wangetakiwa kufukuzwa kazi na kufungwa jela. Hili la Kagera ni dogo sana kwa maana hao askari wapenzi walikubaliana kupiga picha hiyo na kwa umbumbumbu wao waliweka kwenye mitandao. Yapo mambo mengi ya aibu yanafanywa na viongozi na hayakemewi, na yakitokea kwenye jamii yanatetewa.

  5. Mimi naona hao vijana hawana kosa lolote walilofanya hayo ni makubaliano binafsi au kupigana denda ndani ya sare ya jeshi ni kosa basi wekeni wazi kwenye katiba yenu mnayotaka tuipitishe

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles