23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Trafiki waliomtukana dereva, kumpiga watiwa mbaroni

Mwandishi Wetu-Dar es Salaam

ASKARI wawili wa Kikosi cha Usalama Barabarani, ambao wameonekana kwenye video kupitia mitandao ya kijamii wakimtukana dereva na kumpiga yeye na abiria wake,  wamekamatwa na kuwekwa ndani, huku wakisubiri kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Kukamatwa kwao kumetokana na agizo lililotolewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamadi Yussuf Masauni, ambapo alisema Serikali haiko tayari kuona Jeshi la Polisi likichafuliwa na baadhi ya askari waliokosa uadilifu.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam kwenye uzinduzi wa mafunzo ya uchoraji la usalama barabarani, Masauni alisema kumekuwa na malalamiko mengi ya madereva kubambikiwa makosa au askari kufanya vitendo vilivyo kinyume na mwenendo mwema wa jeshi hilo.

Alisema vitendo hivyo vinajumuisha upokeaji wa rushwa, lugha chafu kwa madereva na kuwashambulia, jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

“Jana (juzi) kuna video ambayo ilikuwa ikisambaa kwenye mitandao ya kijamii ikiwaonesha askari wakimtukana dereva na abiria waliokuwamo na si hivyo tu ilifika hadi kumpiga.

“Baada ya tukio hili nilimwagiza Kamanda wa Kiko cha Usalama Barabarani achukue hatua kwa suala hili. Na jana (juzi) ileile nilipewa taarifa wamekamatwa askari waliofanya tendo hilo na wamewekwa ndani na sasa wanasubiri kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

“Hawa askari wapo kituo cha ZTO (Kanda Maalumu ya Dar es Salaam), Serikali haiko tayari kuona raia wake wanaonewa na askari pia anaonewa tunachotaka kila upande ufuate sheria za nchi yetu.

“Nawaomba wananchi wote pindi wanapoona kuna vitendo ambavyo wanafanyiwa ambavyo ni kinyume cha sheria zetu wasisite kutoa taarifa kwetu,” alisema Masauni.

Alisema pindi ikitokea mtumiaji yoyote wa barabara amefanyiwa vitendo vyovyote asisite kuwasiliana na uongozi wa askari aliyefanya vitendo hivyo.

“Na ikitokezea uongozi wa askari husika anatetea au kutochukua hatua muafaka, mlalamikaji apande kwa uongozi wa juu na ikibidi afike hata kwangu nani mitachukua hatua stahiki na utapata mrejesho.

“Kwa msisitiza naomba nizungumze tena tukio la hivi karibuni lilosambaa kwenye mitandao ya kijamii linaloonesha askari wetu, akitoa lugha ya matusi kwa dereva hadi kufikia hatua ya kumshambulia.

“Ninawaasa askari wote kuwa serikali iko makini na haitaruhusu mwananchi yeyote aonewe na vyombo vya dola hali kadhalika hatutaruhusu mwananchi au taasisi yoyote imwonee askari kwa sababu yoyote ile,” alisema.

Akizungumzia suala la usalama barabarani, Masauni aliishukuru Kampuni ya Mafuta ya Puma, kwa kuendesha program hiyo ambapo pia alizitaka kampuni zingine kuiga mfano huo kwa kuwekeza kwenye ulinzi na usalama wa watoto kwani ni Taifa leo kesho na wateja wa kesho pia.

Alisema Jeshi la Polisi kupitia kikosi cha Usalama Barabarani wana program nyingi za kusaidia kutoa mafunzo kwa shule zote zilipo kwenye mazingira hatarishi na zisizo kwenye mazingira hayo pia.

“Programu hizo zimekuwa zikikabiliw na changamoto mbalimbali za kifedha. Ninaomba kutumia fursa hii kuomba uongozi wa Puma kukisaidia Kikosi cha Usalama Barabarani kuzifikia shule zote nchini kwa kupitia askati walioko kwenye maeneo yote nchini.

“Pia ninamwagiza Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani kuanza mchakato wa kuandaa andiko la kutoa mafunzo kwa shule zote nchini na kuliwasilisha kwenu (Puma) ili mwone namna yambavyo mnaweza kusaidia kuokoa kizazi chetu cha kesho,” alisema Masauni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles