25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

TRA yasisitiza wamiliki kulipia kodi ya majengo, malimbikizo

Koku David, Dar es Salaam

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Kodi wa Temeke, imewataka wamiliki wa majengo kulipa kodi hiyo sanjari na madeni ya nyuma.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Jumatano Februari 5, katika semina iliyoshirikisha wamiliki wa majengo wa Kata ya Makangarawe, Meneja wa TRA Mkoa wa Temeke, Paul Walalaze amesema majengo yote yanatakiwa kulipiwa kodi kwa mujibu wa sheria na kwamba kila mmiliki mwenye deni la nyuma anaruhusiwa kulipa taratibu.

Amesema TRA imepewa agizo la kufanya kazi na taasisi za serikali ili kuhakikisha lengo la kukusanya kodi kwa kila anayestahili linafikiwa.

“TRA inamjali mlipa kodi na ndiyo maana imeboresha huduma, lakini pia inapokea maoni na kero za walipa kodi ili kuangalia namna nzuri ya kuweza kuzitatua,” amesema Walalaze.

Kwa upande wake Ofisa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi, Mkoa wa Temeke, Catherine Mwakilagala amesema msamaha wa kodi ya majengo huombwa kila mwaka na mhusika wa msamaha mwenye umri wa kuanzia miaka 60 na zaidi.

Amesema iwapo muombaji wa msamaha huo nyumba yake itakuwa na madeni ya nyuma sheria inamtaka kuyalipa kama kawaida.

“Pia muombaji huyo wa msamaha wa kodi ya majengo anatakiwa kuwa anaishi kwenye nyumba hiyo ambayo yeye ndiye mmiliki halali na si nyumba ya mtoto wake.

“Aidha kuna baadhi ya wazee wanamiliki nyumba mjini na vijijini ambazo zote wanaziombea msamaha, kwa mujibu wa sheria hawaruhusiwi kuombea msamaha nyumba mbili na badala yake atasamehewa nyumba moja tu,” amesema Catherine.

Naye Ofisa Mtendaji wa Kata ya Makangarawe, Baraka Mwasaka amesema wakazi wengi wa eneo hilo hawakuwa na uelewa kuhusu kodi ya majengo hivyo semina hizo zitasaidia kuwaelimisha.

Chiku Sadiki, mkazi wa Kata ya Makangarawe Mtaa wa Abiola amesema elimu hizo zitawasaidia kujua maana ya kodi ya majengo na umuhimu wake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles