31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

TRA yasimamisha washauri sita wawalipa kodi, kupelekwa NBAA kwa hatua za kisheria

KOKU DAVID-DAR ES SALAAM

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imekuwa ikishirikiana kwa karibu na Jukwaa la Washauri wa Kodi (TTPF) katika kuhakikisha inafanikisha lengo lake la ukusanyaji wa mapato.

Wataalamu hao ni wadau muhimu kwa TRA kutokana na kuwa wana nafasi kubwa ya kuwa karibu na walipakodi ambao wana haki ya kuwakilishwa kwa mujibu wa sheria.

Sambamba na kuwakilisha walipakodi, washauri wa kodi hutumika kuwasaidia walipakodi katika kutengeneza vitabu pamoja na kufanya ritani kwaajili ya kulipa kodi.

 Hata hivyo kwa mujibu wa TRA, kuna baadhi ya washauri wa kodi ambao wamekuwa sio waaminifu na badala yake wanakiuka maadili na kuifanya mamlaka hiyo kukosa kodi stahiki.

Kamishna Mkuu wa TRA, Charles Kichere anasema kuwa washauri wa kodi ni wadau muhimu katika suala zima la kuisaidia serikali kuweza kupata mapato yake stahiki.

Anasema kwa kushirikiana na washauri wa kodi, TRA itaweza kukusanya mapato hadi kufikia lengo walilo wekewa na serikali.

Anasema katika kuhakikisha malengo ya kushirikiana katika suala la ukusanyaji wa kodi linafanikiwa, mwisho mwa wiki iliyopita mamlaka hiyo ilikutana katika semina ya siku moja na washauri wa kodi ili kubadilisha mawazo pamoja na kuangalia namna nzuri ya kuweza kutatua changamoto mbalimbali zilizopo.

Kichere anasema moja ya changamoto ni baadhi ya walipakodi kuwa na vitabu viwili kwa mwaka mmoja wa fedha ambapo vile vyenye faida kubwa wanadai ni kwaajili ya kuombea mkopo benki na vyenye faida ndogo vinapelekwa TRA kwaajili ya kulipia kodi.

Anasema kutokana na hali hiyo wanaikosesha serikali mapato stahiki na kwamba suala hilo ni moja ya ajenda iliyojadiliwa katika semina hiyo ambayo lengo lake ilikuwa ni kutafuta namna nzuri ya kutatua changamoto hizo.

Anasema wamekuwa kiwachukulia hatua za kisheria baadhi ya washauri wa kodi ambao wamekuwa wakiikosesha serikali mapato na kwamba hadi sasa washauri sita wameshachukuliwa hatua kwa kupelekwa katika Bodi ya Uhasibu na Ukaguzi wa Hesabu (NBAA) kwaajili ya hatua za kisheria.

Kichere anasema mlipakodi kuwa na vitabu viwili ndani ya mwaka mmoja wa fedha ni kukiuka sheria na kwamba ukiukaji huo wa maadili unasababisha kushuka kwa ukusanyaji wa kodi.

Anaongeza kuwa kutosaidia kutekeleza wajibu wa kisheria kunakofanywa na baadhi ya washauri wa kodi ni ukiukaji wa maadili ambao unatakiwa kuchukuliwa hatua.

Anasema hatua ya kwanza inayochukuliwa dhidi ya washauri wa kodi wanaokiuka maadili kuwapeleka NBAA ambako uchunguzi utafanyika ili kubaini sababu iliyowafanya kukiuka madili.

Anasema washauri wa kodi ni watu muhimu katika masuala ya kukusanya kodi kutokana na kuwa wanawasaidia walipakodi kutengeneza vitabu na kufanya ritani kwaajili ya kulipa kodi hivyo TRA inatakiwa kushirikiana nao kwa ukaribu.

Anasema washauri wa kodi wanatakiwa kuisaidia serikali katika kukusanya kodi stahiki ikiwa ni pamoja na kuwasaidia walipa kodi kutengeneza vitabu stahiki hasa ukizingatia kuwa sheria inampa mlipakodi haki ya kuwakilishwa.

Kichere anasema kuwa waziri ana mamlaka ya kutunga kanuni za kuwasimamia washauri wa kodi ambazo kamisha ndiye anayezisimamia.

Sambamba na kuzisimamia kanuni hizo, pia kamishna amepewa nguvu ya kuwafuta katika daftari la wataalamu la washauri wa kodi watakaokiuka maadili.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles