24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

TRA tunawakaribisha Wananchi Sabasaba kupata elimu

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imesema imejipanga kuhakikisha inatoa elimu, kupokea maoni pamoja na kutoa huduma mbalimbali kwa wananchi watakaotembelea banda la TRA katika maonyesho ya 45 ya sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.

Akizungumza jijini hapa jana katika banda la TRA Sabasaba, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi wa TRA, Richard Kayombo amesma katika banda la mamlaka hiyo wananchi watapata nafasi ya kujifunza taratibu mbalimbali za ulipaji wa kodi, kujifunza huduma zinazotolewa kwa njia ya mtandao, pamoja na idara mbalimbali kutoka ndani ya mamlaka.

Amesema pia wananchi wanaweza kupewa maelezo ya namna wanavyoweza kutumia tovuti ya TRA katika kupata taarifa mbalimbali zitakazomuwezesha kuelimika.

“Pia wanaweza kupata huduma ya mnada kwa njia ya mtandao ambayo tungependa wananchi wajifunze namna ya kuitumia, lakini pia tungependa wananchi watupe maoni ya kujenga kuwa ni kitu gani wangependa turekebishe ili tuwajengee utayari wa kulipa kodi kwa hiyari.

“Maonyesho yameanza tangu Juni 28 na yatamalizika Julai 13 na kwamba wananchi pia watapata nafasi ya kujifunza mambo ya kiforodha kama vile kupata maelezo kuhusu vituo vya pamoja Mpakani ambavyo hivi sasa vipo kama nane katika nchi jirani na nchi za SADC,” amesema Kayombo.

Amesema kodi ni msingi wa maendeleo na kwamba TRA inazingatia kauli mbiu ya kukuza uchumi wa viwanda ili kuongeza ajira na biashara ikiwa ni pamoja na kuzingatia kauli na miongozo ya viongozi wakuu wa nchi kwa kuwatoza wananchi kodi stahiki bila kuwaonea.

Naye Adelaida Rweikiza ambaye ni Afisa Maadili Mwandamizi amesema wananchi watakaotembelea banda la TRA idara ya mambo ya ndani watapata nafasi ya kujua namna wanavyosimamia maadili kwa watumishi wake na kwamba maadili ndio msingi wa mamlaka lakini pia katika tovuti ya mamlaka mtu anaweza kutoa taarifa za uvunjifu wa maadili utakaofanywa na watumishi na kwamba taarifa hiyo itamfikia moja kwa moja Kamishna Mkuu pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Maadili kwa wakati.

Kwa upande wa mteja aliyejitambulisha kwa jina la Amina Ally amesema kuwa huduma zinazotolewa na TRA katika maonyesho ya kimataifa ya 45 sabasaba ni nzuri na za haraka na kwamba wananchi au wafanyabiashara wenye uhitaji wa kuhudumiwa wafike ili wahudumiwe haraka.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles