Na MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM
SHIRIKA la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), limefikia makubaliano na Kampuni ya Saruji ya Dangote kuuziana gesi asilia kwa matumizi ya kiwanda hicho kilichoko mkoani Mtwara.
Makubaliano hayo yamefikiwa ikiwa ni wiki moja tangu Rais Dk. John Magufuli aliagize shirika hilo kufikia mwafaka na Kampuni ya Dangote juu ya mauziano ya gesi asilia.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa shirika hilo, Kapulya Musomba, alisema jana kuwa makubaliano hayo yanahusu kuunganisha miundombinu ya kusafirisha gesi asilia toka katika bomba kubwa la gesi kwenda kiwandani hapo.
Alisema kazi ya kuunganisha miundombinu ya gesi asilia katika mitambo ya kufua umeme utakaotumiwa na kiwanda hicho inatarajia kuanza mara moja.
Machi 5 mwaka huu, wakati Rais Magufuli alipokwenda kiwandani hapo kuzindua magari ya kampuni hiyo, alimtaka mmiliki wa kiwanda hicho, Aliko Dangote, kununua gesi kutoka TPDC badala ya kutumia watu wa kati ambao wana lengo la kutengeneza faida zaidi.