31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Tido Mhando asimulia wafanyakazi Azam walivyopata ajali

Bethsheba Wambura, Dar es Salaam

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Azam Media Ltd, Tido Mhando amesimulia jinsi wafanyakazi walivyoondoka ofisini kuelekea Chato mkoani Geita kikazi kabla ya kutokea ajali iliyokatisha uhai wao na namna uongozi ulivyopokea taarifa za vifo hivyo.

Wafanyakazi watano wa Azam Media walifariki katika ajali ya agri iliyotokea kati ya Shelui na Igunga jana Julai 8, iliyouhisha gari aina ya Toyota Coaster iliyogongana uso kwa uso na lori ambapo pia dereva wa Coaster na utingo wake walipoteza maisha papo hapo.

Akielezea tukio hilo leo Jumane Julai 9, wakati miili ya wafanyakazi hao ikiagwa katika Ofisi za Azam, Tabata jijini Dar es Salaam, Tido amesema alipopigiwa simu Jumapili Julai 7, na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (Tanapa) za kuomba wafanyakazi wa Azam Media kwenda kuonesha matangazo ya moja kwa moja katika uzinduzi wa Hifadhi ya Burigi-Chato, ilikuwa ngumu lakini alipowaambia wafanyakazi hao walikubali kwenda.

“Tumekuwa tukipata mialiko ya kufanya kazi nyingi za kitaifa na tunazifanya kama inavyotakiwa, Jumapili tulipata taarifa kutoka kwa wenzetu wa Tanapa wakitaka tushirikiane nao katika tukio kubwa la uzinduzi wa hifadhi kule Chato ambao umefanyika leo, kwa haraka tukajipanga kutafuta watu.

“Huwezi kuamini Mtendaji kama mimi siku ya Jumapili kuweza kufanikiwa kuwapata watu haraka haraka waweze kuondoka, watu wana mambo yao kama wale vijana wana shughuli zao lakini haikuwa hivyo kwetu sisi viongozi tulipopitisha neno moja tu kwa vijana hawa wakajipanga wakaondoka na huo ndiyo utaratibu na utayari wao siku zote,” ameeleza Mhando.

Mhando ameendelea kueleza baada ya kutokea ajali hiyo namna wao kama viongozi walivyopokea taarifa za msiba wa wafanyakazi wao kwa mshtuko mkubwa.

“Sisi tulipopata taarifa tulikuwa katika kikao cha kawaida tu cha Jumatatu cha menejinenti tukizungumza mambo mengine ndipo tulipopata taarifa kutoka kwa msamaria mwema aliyeshuhudia ajali hiyo, tulikuwa na kundi la watu 10 ambapo wafanyakazi wetu ni wanane na dereva na utingo wake lakini kwa wakati huo hakuna hata mmoja ambaye angeweza kuelezea kilichotokea hapo ndipo tuliona hii siyo hali ya kawaida.

“Tulipata mshtuko mkubwa sana kwa kweli, pamoja na kwamba tumezoea kukutana na kuzungumzia masuala mbalimbali ya kiuongozi lakini ilituchukua saa mbili tukitafakari tuzungumze kuhusu nini, hatujui wapi pa kuanzia lakini hatimaye tulipata nguvu tukijua huu ni wajibu wetu ili wapendwa wetu hawa tuwalaze vizuri na tuwape kila heshima wanayostahili,” ameeleza Mhando.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles