NA, MURUGWA THOMAS,TABORA.
WANANCHI mkoani Tabora, wametakiwa kujenga tabia ya kutafuta tiba kwenye vituo vya afya, badala kwenda kwa wanganga wa kienyeji.
Kauli hiyo, ilitolewa na Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma Mkoa wa Tabora,Dk. Benedict Komba,ukiwa ni ujumbe wake kwa wananchi wakati wa maadhimisho ya siku ya kifua kikuu duniani jana.
Alisema kifua kikuu kinatibika, lakini wagonjwa wengi wamepoteza maisha wakiwa wamechelewa kupata tiba na kusababisha ugonjwa kuwa sugu.
Alisema ugonjwa huo, unaongoza kwa vifo vya watu,ukifuatiwa na mangonjwa mengine kama homa ya ini na mapafu, Ukimwi na maralia.
Alisema licha ya ugonjwa huo kutibika, takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO), zinaonyesha zaidi ya watu 50 hupoteza maisha kila siku nchini.
Alisema wananchi wengi mkoani hapa, wamekuwa wakianzia kwa waganga wa kienyeji kupata tiba na kujikuta wakichelewa kufika vituo vya afya kupata tiba sahihi.
Alisema tamaduni na mila mila potofu zikiambatana na imani za kishirikina ndiyo sababu kubwa inayowafanya wagonjwa wengi kupoteza maisha.
Alisema takwimu za mwaka 2018/19, wagonjwa 314 walipoteza maisha kutokana na kufika hospilali wakiwa wamechelewa kupata tiba.
Alisema ugonjwa upo ndani ya jamii na kasi ya kuendelea kubaini maabukizi mapya, imeongezeka kutokana na elimu wanayotoa kwa ushirikiano wa viongozi wa Serikali na vyombo vya habari.
Mkazi wa Manispaa ya Tabora, Sadda Kaswa aliwaasa wanachi kutowanyanyapaa wagonjwa kwa sababu ugonjwa huo unatibika.
Ofisa muuguzi msaidizi anayehudumu kliniki ya TB Hospitali ya Rufaa ya Kitete, Dafrosa Simon aliwaasa wagonjwa na waangalizi wao kufuatilia kalenda ya matibabu ili kujiepusha kupata madhara, ikiwamo kupoteza maisha.
Siku ya kifua kikuu uadhimishwa duniani kote Machi 24 kila mwaka na ambapo kwa mwaka huu maadhimisho hayo yanafanywa na watumishi wa kada ya afya kutoa jumbe mbali mbali kwa wananchi jinsi ya kuzuia maambukizi na tiba kwa waaathirika.