Mwandishi wetu,Dar es Salaam
Mtandao wa Jinsia nchini (TGNP), umeandaa mafunzo yenye lengo la kutoa hamasa kwa wanawake wote wenye hofu na woga wa kushiriki katika kuweka nia kwenye ngazi za uongozi wa uchaguzi mdogo wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.
Mafunzo hayo yamefanyika leo Jumanne Oktoba 29, katika Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani, ambapo Schola Makyaiya kutoka shirika hilo amewataka wanawake hao kuacha uoga na badala yake wawe walimu kwa wanawake wengine.
“Wanawake wengi katika karne hii wanaogopa sana kushiriki katika kugombea nafasi za uongozi kwahiyo baada ya mafunzo haya naomba mkawe walimu wa kutoa mafunzo kwa wale wote ambao hawakushiri katika mafunzo haya ,”amesema.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kisarawe, Alphan Kisa amesema asilimia 90 ya wanawake kwa mwaka huu hasa katika wilaya hiyo wamejitokeza katika kugombea nafasi ya uenyekiti wa mitaa,na vitongoji.
Naye Katibu wa Chama Cha Wananchi CUF Wilaya ya Kisarawe, Omari Ally amesema changamoto zilizopo kwa wanawake katika kujitokeza kugombea uongozi ni hofu ya ushiriki kugombea na kutokuwa na ujasiri wa kusimama mbele za watu na kuongea.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Kisarawe, Alphonce Mayugane amesema kwa upande wa chama hicho wanawake wamejitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi.