27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

TGNP: Wanawake nguzo imara kuleta maendeleo nchini

OSCAR ASSENGA, MUHEZA

KATIKA Taifa lolote lile, wanawake huwa ni nguzo ya jamii na nchi kwa ujumla.

Siku zote, ukiacha juhudi alizonazo katika kuhakikisha familia yake haiteteleki, amekuwa ni nguzo imara katika kukuza uchumi wan chi.

Jambo ambalo huwakwamisha ni woga walionao katika kuwania nafasi mbalimbali za uongozi, hii inatokana na kudharauliwa kwao na baadhi ya wanaume wakiwaona kuwa hawawezi kuongoza nchi wala eneo lolote lile katika jamii inayowazunguka.

Ili kuondoa kabisa dhana hii, ni wajibu wao kuwa mstari wa mbele katika kuwania nyadhifa mbalimbali katika jamii, wasiogope kushindwa bali wajitose wakiamini wanaweza.

Tumeshuhudia viongozi wanawake waliopita na waliopo sasa jinsi walivyosaidia kuleta maendeleo katika Taifa hili, ili kuendeleza ujasiri huu ni muhimu na wengine wengi wajitokeze kuwania nyafidha za uongozi nchini.

Ofisa Programu Harakati na Ujenzi wa Pamoja kutoka Mtandao wa Kijinsia Tanzania (TGNP), Anna Sangai, anasema mwanamke anaweza kuwa rais na nchi ikaendelea vizuri kwa sababu ni waadilifu na huwa wanafanyakazi kwa juhudi kubwa.

Huku akitolea mfano uadilifu wao ulivyokuwa madhubuti hata wakati wa utumbuaji, wanawake walikuwa ni wachache ukilinganisha na wanaume hivyo wanaweza kushika nafasi hiyo ya juu kwenye nchi kutokana na uadilifu wao.

Akiwa katika semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari kuripoti habari za jinsia, aliwataka wanawake kuwa mstari wa mbele kugombea nafasi mbalimbali kwenye chaguzi ili kushirikiana na jamii kusaidia kuleta maendeleo.

“Ndugu zangu tusiwe tunaogopa kuwania nafasi za uongozi, hakuna jambo linalowashinda wanawake, ni vema waone umuhimu wa kuwania uongozi wowote katika Taifa hili,”anasema.

Anaongeza: “Tuna nafasi kubwa ya kushiriki kwenye chaguzi mbalimbali nchini, tunaona jinsi ambavyo Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan anavyotuongoza vizuri, inawezekana mwanamke akawa rais na nchi ikaendelea vizuri kwa sababu ni waadilifu na wachapa kazi,” anasema.

Akizungumzia athari za mfumo dume kwenye jamii, anasema kwamba ni kubwa kwa sababu inagusa maeneo mengi ya kichumi, kijamii, upatikanaji wa huduma za jamii huku akieleza jamii inatakiwa kutambua kwamba eneo ambalo kuna hali hiyo hata maendeleo yatachelewa kupatikana.

Anasema kwa kawaida mfumo dume huwa unaathiri uchumi na kudidimiza maendeleo, akitolea mfano pale wanawake wanapohitaji nafasi ya kushiriki kwenye uchumi unakuta mfumo unaonyesha hawatakiwi kufanya hivyo na badala yake wanakaa nyumbani kwa hiyo, wanapokaa nyumbani kwenye eneo la uchumi umaskini unaendelea. Wanaamini kuwa wanawake wapo wengi zaidi ya asilimia 50 hivyo wanaposhiriki kwenye suala la uzalishaji mali huwa wanaongeza kipato cha familia na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Ofisa Habari Mtandao wa Kijinsia Tanzania (TGNP), Monica John, anasema mfumo dume upo kwenye jamii na wakati mwingine unatokana na nguvu aliyokuwa nayo mtu katika hali ya kumiliki rasilimali na kutoa uamuzi.

Anasema sehemu kubwa kwenye jamii mfumo dume unasababishwa na  wanaume kuwanyima sauti wanawake katika kuongeza vitu na hata kumiliki rasiliamali, lakini pia upo kwenye pande mbili kwa sababu athari zake wakati mwingine hutokea pande zote mbili.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles