31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

TCU, WANAFUNZI ST, JOSEPH KUSULUHISHWA FEBRUARI 15

Na Kulwa Mzee-Dar es Salaam

USULUHISHI kesi ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha St. Joseph waliorudishwa nyumbani kwa kukosa sifa kutokana na vigezo vya Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kufanyika Februari 15 mwaka huu.

Mahakama Kuu inatarajia kufanya usuluhishi huo katika kesi ya madai ya Sh bilioni 6 iliyofunguliwa na wanafunzi 316 waliokuwa wakisoma chuo hicho.

Awali usuluhishi ulitakiwa kufanyika Januari 23 mwaka huu mbele ya Jaji Rose Temba, lakini ulipangiwa tarehe nyingine ambapo sasa utafanyika Februari 15 kwa sababu ya kusubiri mwongozo kutoka kwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako.

Katika usuluhishi huo, wizara hiyo inawakilishwa na wakili Anna Kalomo  ambaye aliomba waziri huyo aipitie na atoe mwongozo wake ili maamuzi mazuri yaweze kufikiwa.

TCU inawakilishwa na Rose Rutha, St. Joseph  inawakilishwa na wakili Jerome Msemwa huku wanafunzi wakiwakilishwa na wakili, Emmanuel Muga.

Kwa utaratibu wa mahakama endapo usuluhishi huo utashindikana,  kesi ya msingi ambayo ipo mbele ya  Jaji Winfrida Koroso itaanza kusikilizwa.

Katika kesi hiyo, wanafunzi wanne Ramadhan Kipenya, Inocent Peter , Faith Kyando na Mohammed Mtunguja waliruhusiwa kuwawakilisha wenzao mahakamani hapo.

Wanafunzi hao ambao wanatetewa na wakili Muga wanaiomba mahakama hiyo iamuru walipwe zaidi ya Sh bilioni 1 kama gharama ikiwamo za ada walizokilipa chuo hicho.

Pia wanaomba kulipwa Sh bilioni 5 kama fidia ya jumla ya  gharama za  hasara  walizozipata.

Wakili Muga aliiomba mahakama kuendesha kesi hiyo kwa haraka kwa sababu wanafunzi hao wapo mtaani na hawajui hatima yao na fedha zao zimeliwa.

Katika kesi hiyo, wanafunzi hao kupitia wakili wao wanadai kuwa TCU iliruhusu Chuo Kikuu cha St. Joseph kudahili wanafunzi wa digrii ya miaka mitano wa ualimu wa Sayansi.

Miaka miwili kwa ajili ya kuwaweka wanafunzi hao vizuri kwa sababu ni wa kidato cha nne  lakini baadaye Mei 2016, TCU ikasema hawana sifa warudi nyumbani wakati baadhi yao walikwisha kaa  chuoni hapo kwa kipindi cha mwaka mmoja, miwili na wengine mitatu na wamekwisha kilipa gharama nyingi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles