24.4 C
Dar es Salaam
Thursday, September 19, 2024

Contact us: [email protected]

TARURA Mkoa wa Pwani yasaini mikataba ya ujenzi wa Barabara yenye thamani ya Bilioni 31.4

Na Gustaphu Haule, Mtanzania Digital

Kibaha. Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini Tanzania (TARURA) Mkoa wa Pwani, imeingia mikataba na wakandarasi mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa barabara zenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 31.4. Hafla ya utiaji saini imefanyika leo, Agosti 19, 2024, mjini Kibaha, na kushuhudiwa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa halmashauri, watumishi wa TARURA, wawakilishi wa taasisi za kibenki, na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini, Silvestry Koka.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge akipokea mikataba ya ujenzi wa barabara kutoka kwa meneja Tarura Mkoa wa Pwani Leopold Runji katika hafla ya utiaji saini wa mikataba ya ujenzi wa barabara kwa mwaka 2024/2025 iliyofanyika Agosti 19,2024 Mjini Kibaha.

Meneja wa TARURA Mkoa wa Pwani, Mhandisi Leopold Runji, amesema mikataba hiyo itatekelezwa katika mwaka wa fedha 2024/2025, na fedha zitatoka katika vyanzo mbalimbali, ikiwemo Shilingi bilioni 7.5 kutoka Mfuko wa Barabara (Road Fund), Sh bilioni 14.5 kutoka tozo ya mafuta, Sh bilioni 4.5 kutoka Mfuko wa Jimbo, Sh milioni 300 kwa miradi ya maendeleo ya barabara, na Sh bilioni 1.9 kutoka Mfuko wa Dharura.

Awamu ya kwanza ya mikataba hiyo imejumuisha mikataba 25 yenye thamani ya Sh bilioni 11.6, ambayo ni asilimia 37 ya bajeti ya mwaka 2024/2025. Awamu ya pili itahusisha mikataba iliyosalia.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge, amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za utekelezaji wa miradi hiyo, na kupongeza TARURA na TANROADS kwa usimamizi mzuri wa fedha na utekelezaji wa miradi ya barabara ndani ya Mkoa wa Pwani.

Kunenge amewataka wakandarasi kuhakikisha wanatekeleza miradi kwa mujibu wa mikataba yao, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano na usimamizi wa karibu kutoka kwa viongozi wa wilaya na wananchi ili kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa.

Wakandarasi wa kampuni ya ujenzi wa barabara ya Old South iliyopo Mjini Kibaha wakibadilishana hati ya mikataba na meneja wa Tarura Mkoa wa Pwani, Leopold Runji katika hafla ya utiani saini mikataba hiyo iliyofanyika leo Mjini Kibaha.

Pia, amewataka wananchi kushirikiana na serikali katika kutunza miundombinu ya barabara, na kuhakikisha taarifa za uharibifu zinatolewa mapema ili hatua zichukuliwe haraka.

Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini, Silvestry Koka, amemshukuru Rais Samia kwa jitihada zake kubwa katika kuboresha sekta zote muhimu, ikiwemo barabara, maji, afya, elimu, na umeme, na kusisitiza kuwa fedha hizo zitasaidia kuboresha barabara zilizoharibika na hivyo kurahisisha maisha ya wananchi katika kufanya shughuli zao za kiuchumi.

Wadau wa barabara akiwemo mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka wakishuhudia hafla ya utiaji saini wa mikataba ya ujenzi wa barabara ya mwaka 2024/2025 iliyofanyika leo Agosti 19 katika jengo la ofisi ya Mkuu wa Mkoa lililopo Kibaha Mjini.
- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles