Ramadhan Hassan,Dodoma
Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania umeeleza kuwa tangu ipewe mamlaka na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kutafiti na kuzalisha chanjo, chanjo milioni 65 za mifugo kama ng’ombe, kuku, kondoo, mbuzi na mbwa zimezalishwa.
Pia imesema asilimia 65 ya vifo vya ng’ombe vinasababishwa na mdudu kupe.
Hayo yameelezwa leo Oktoba 21,2022 na Mtendaji Mkuu wa Wakala huo, Dk. Stella Bitanyi wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa Habari kuhusu utekelezaji na mwelekeo wa bajeti ya Maabara hiyo kwa mwaka 2022-2023.
Dk. Stella amesema tangu Maabara hiyo ipewe mamlaka na Wizara ya mifugo na uvuvi kutafiti na kuzalisha chanjo, chanjo 65 milioni za mifugo kama ng’ombe, kuku, kondoo, mbuzi na mbwa zimezalishwa.
Aidha, pia amesema asilimia 65 ya vifo vya ng’ombe vinasababishwa na mdudu kupe.
Amesema mdudu huyo anayesababisha magonjwa makuu mawili, asilimia 80 kati ya vifo hivyo vinatokana na aina ya ugonjwa wa ndigana kali ukilinganisha na ndigana baridi.
Amesema ugonjwa huo unaongoza kuua ng’ombe na ni gharama zaidi katika matibabu yake.
Amesema magonjwa yote ya wanyama yanaua ila inategemea yametokea kwa kipindi gani kwasababu kuna magonjwa ya mlipuko ambayo huua Kwa kasi na kwa wakati mmoja.
“Lakini huu ugonjwa upo siku zote na unaathiri sana na una gharama katika matibabu yake,” amesema Dk. Stella
Mtendaji huyo amesema Wizara ipo katika mpango wa kuhakikisha kuwa kila Kata na Kijiji kinakuwa na josho na kutoa dawa za kuogeshea mifugo zinazotokana na ruzuku kutoka serikalini.