25 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Tani 900 za mbolea zaanza kusambazwa Katavi

Na WALTER MGULUCHUMA-KATAVI


WAKULIMA Mkoa wa Katavi  wamekunwa na hatua  ya kuanza  kusambazwa  kwa  tani zaidi ya 900 za mbolea  ya  mahindi na  tumbaku,  itakayosaidia  kuongeza uzalishaji wa mazao hayo katika  mkoa  huo.

Wakala  mkuu wa  kusambaza na kuuza  pembejeo, Yara, tayari amefungua ghala  kubwa la kuhifadhi  mbolea katika  Mkoa wa  Katavi   lenye uwezo wa kuhifadhi   tani 4,000.

Kaimu  Katibu   Tawala wa  Mkoa wa  Katavi,  Crisencia  Joseph, ambaye  alimwakilisha  Mkuu wa  Mkoa wa  Katavi kwenye uzinduzi wa  ghala  hilo,  alisema mkoa  umefarijika  kuona mbolea ikiwa imeingia  kwa wingi  na zaidi  tayari  imehifadhiwa  kwenye  ghala   ikisubiri msimu wa kilimo kuanza.

Crisencia  alieleza  kuwa  katika msimu uliopita kulikuwa na changamoto  mbalimbali ikiwamo mbolea kutofika kwa wakati kwa wakulima, baadhi ya  mbegu kutoota na wadudu  wa kuharibu  mazao.

Alitoa wito kwa msimu huu wakulima kuzalisha  mazao  kwa wingi  kwa kuwa pembejeo  zimewahi kuwafikia.

Naye Bwana  shamba  Mkuu wa  Yara,  Peter Assey,  alisema wao si  wanauza  mbolea  tu bali   wanawekeza  katika  mnyororo  wote  wa kuongeza   thamani  ya mazao  kwa kuanzisha vituo  vikubwa  vitano  katika maeneo ya  Moshi,  Iringa,  Mbeya, Njombe, Morogoro na  sasa    Katavi  Wilaya ya  Mpanda.

Mkurugenzi wa   Wakala  Mkuu wa    Yara wa  Nyanda za  Juu,  Olais  Oleseenga,  alisema  hadi sasa  jumla ya tani 940 za  mbolea   tayari zimeshafikishwa  mkoani  Katavi huku  tani 80  kati ya  hizo ni  mbolea za  tumbaku na  tani nyingine  ni za  mahindi.

Alifafanua kuwa  lengo  la  Yara  ni  kupeleka  tani  4,000  na kuzihifadhi kwenye  ghala  hilo la  Mpanda  na tani 2,000  kati ya  hizo  zitasafirishwa kwenda mkoani  Rukwa.

Alisema wamebaini kusafirisha  mbolea kwa kupitia  Mpanda  kwenda   Sumbawanga, gharama zake  ni nafuu kuliko kupitia  mkoani  Mbeya.

Akizungumzia malengo ya mwakani, alisema wanatarajia  kupeleka  mbolea  wilayani   Kasulu  mkoani  Kigoma  kwa kupitia Mpanda kwani kuna  usafiri wa kutumia  treni  hadi  Mpanda kutokea  Dar es Salaam  na hivyo kufanya bei ya mfuko wa mbolea wa kilo 50 kushuka  kwa thamani ya  shilingi  4,000  na kumpa nafuu mkulima.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles