30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Tanesco yaokoa bil 6.8/- ujenzi wa gridi ya Taifa Mpanda

MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Umeme Tanzania (Tanesco), limesema kuwa hatua ya kujengwa kwa mradi wa umeme wa megawati 132 mkoani Katavi, ambao utaokoa zaidi ya Sh bilioni 6.8 zilizokuwa zikitumika kununua mafuta kwa ajili ya majenereta ya kufua umeme.

Hata pia baada ya kukamilika kwa mradi huo Tanesco ikianza kuuza umeme watapata zaidi ya Sh bilioni 1.4 kwa mwezi ambapo awali kwa kituo cha Mpanda pekee walikuwa wakitumia Sh milioni 800 kwa ajili ya kununua mafuta.

Hatua hiyo inatajwa kuwa ni sehemu ya mageuzi makubwa yanayofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dk. John Magufuli ya kuhakikisha nchi inakuwa na umeme wa uhakika na kuwa na uchumi wa kati na wa viwanda.

Akizundua mradi mwishoni mwa wiki iiyopita Rais Magufuli alifichua siri ya kuwepo mgao wa umeme nchini kabla hajaingia madarakani mwaka 2015, alisema ulitokana na baadhi ya wafanyakazi wa Tanesco ambao walikuwa wakifungulia maji kwenye Bwawa la Mtera ili likauke.

Alisema lengo la wafanyakazi hao ilitokana na kula njama na wafanyabiashara waliokuwa wanauza jenereta ili wawape fedha.

 “Dar es Salaam ilifika kipindi kila mtu ana jenereta yaani Dar nzima ikawa inanuka Petroli na Diseli, kwa sababu umeme ulikuwa wa mgao, sasa tulipoingia madarakani tukasema lazima tuupige marufuku huu mgao kwa njia mbadala na ndio maana tukaongeza production ya umeme.

“Pale kwenye Bwawa la Mtrera mvua zilivyokuwa zikinyesha kuna watu walikuwa wanafungulia maji yatoke na baada ya mwezi mmoja wanakwambia maji yamekauka kumbe walikuwa wanalipwa hela na hawa watu wa majenereta,” alisema Rais Magufuli.

Kutokana na hilo, alisema alimwagiza Waziri wa Nishati, Dk. Medard Kalemani awatumbue wote na baadaye maji hayajakauka katika bwawa hilo.

Mbali na hilo, pia alisema Serikali ilikuwa ikitoa ruzuku ya Sh bilioni 200 kila mwaka kwa ajili ya Tanesco kujiendesha na bado kukawa na mgao, lakini alipoingia madarakani shirika hilo haijawahi kupewa fedha na mgao umeisha.

“Tanesco, Serikali ilikuwa ikitoa ruzuku ya Sh bilioni 200 kwa mwaka badala ya kuzipeleka kwenye hospitali na huduma zingine lakini zilikuwa zikitolewa Tanesco na bado mgao ulikwepo.

“Tanesco napo kulikuwa na majipu, tukatumbua sasa hatupeleki hata senti tano na umeme unawaka, hakuna mgao tena na katika hilo miradi ya Tanesco sasa imesambaa, wakati tunaingia madarakani vijiji vilivyokuwa vimepelekewa umeme vilikuwa 2000 lakini sasa ni zaidi ya vijiji 8100.

“Ni kweli mkoa mpya wa Katavi umekuwa na tatizo la umeme na kwa dunia ya leo na kwa nchi ninayo plan (ninayopanga) ya viwanda huwezi ukawa na umeme wa jenereta.

“Matumizi ya mafuta kwa ajili ya kuwasha jenereta ili utengeneze umeme yamekuwa makubwa ni Sh bilioni 6.5 kila mwaka inapotea na makusanyo ni Sh bilioni 1,” alisema Rais Magufuli.

Mbali na mradi huo, Rais Magufuli alisema kuna miradi mingine ya umeme ukiwemo wa umeme wa bwawa la Nyerere lililoko katika pori la akiba la Selous mkoani Pwani litakalozalisha megawati 2,115,

Mwingine ni mradi wa gridi ya Taifa utakaounganishwa kutoka Zambia utakaozalisha megawati 400 na kupita Katavi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles