30.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

TALGWU YAWASHUKIA WAKUU WA MIKOA, WILAYA

Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU), Rashid Mtima, akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, kulaani matumizi mabaya ya madaraka ya baadhi ya viongozi wa Serikali dhidi ya watendaji wa vijiji, mitaa na kata. Kushoto ni Naibu Katibu mkuu wa chama hicho, Obadia Mwakasitu.
Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU), Rashid Mtima, akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, kulaani matumizi mabaya ya madaraka ya baadhi ya viongozi wa Serikali dhidi ya watendaji wa vijiji, mitaa na kata. Kushoto ni Naibu Katibu mkuu wa chama hicho, Obadia Mwakasitu.

Na MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM

CHAMA cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU) kimevunja ukimya na kuwataka viongozi wa Serikali,  hasa wakuu wa mikoa na wilaya kuacha mara moja kutumia madaraka yao vibaya dhidi ya wafanyakazi.

TALGWU imesema kuwa viongozi hao wamekuwa wakitumia kile wanachodai utumbuaji kwa watendaji kiuonevu na ukiukwaji sheria za nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa TALGWU, Rashid Mtima, alisema baadhi ya viongozi wa kisiasa wamekuwa wakitumia nafasi hiyo kama njia ya kujipatia sifa ama kuonyesha mabavu ya mamlaka yao.

Alisema viongozi hao wamethubutu kutumia vibaya nafasi zao kwa kuendeleza manyanyaso kwa wafanyakazi wa kada ya watendaji wa vijiji, mitaa na kata, wakiwaadhibu bila kufuata utaratibu wa kiutumishi, huku mamlaka zinazopaswa kutumika kwa kazi hiyo zikiporwa madaraka yake kwa nguvu ya kisiasa.

“Jambo hili ni baya na la hatari kwa mujibu wa mustakabali wa utawala wa sheria na linapaswa kukemewa mara moja na kwa nguvu zote kwa sababu likiachwa lina madhara makubwa.

“Tumeshuhudia matukio ya udhalilishaji na ukiukwaji wa taratibu za kazi wakifanyiwa kada hii, maofisa watendaji wamekuwa wakiwekwa ndani ovyo kana kwamba wametenda makosa ya jinai, kutukanwa na kudharauliwa hadharani na wanasiasa, kusimamishwa kazi ovyo bila kuzingatia mamlaka zao za ajira.

“Kwa mfano Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Hapi, aliwaweka ndani watendaji wanne wa Kata ya Mikocheni kwa kushindwa kutekeleza maagizo yake, vilevile Hapi alipotembelea Kata ya Kawe aliwaweka ndani watendaji watatu wa mtaa kwa kosa la kuwapa mashine za kukusanyia fedha wakandarasi na kutounda vikundi vya ulinzi shirikishi,” alisema Mtima.

Katibu mkuu huyo alisema kuwa sheria ya tawala za mikoa ya mwaka 1997 inampa mamlaka mkuu wa mkoa katika kifungu cha 7 (1) hadi (9) na mkuu wa wilaya katika kifungu cha 15 (1) hadi (9) ya kuamrisha mtu yeyote kuwekwa ndani kwa kuona mbele yake au ufahamu wake mtu huyo kuwa ametenda kosa.

Alisema kifungu kidogo cha (2) cha sheria hiyo kinamtaka mkuu wa mkoa au wilaya kufanya hivyo pale ambapo atakuwa amejihakikishia kuwa kosa lililotendwa na mhusika ni lazima litasababisha uvunjivu wa amani kwa mtendaji na jamii kwa jumla na hakuna njia mbadala zaidi ya kumuweka ndani.

“Pia kifungu (3) kinamtaka mtu aliyekamatwa kwa amri au maelekezo ya mkuu wa mkoa au wilaya afikishwe mahakamani ndani ya saa 48 kwa ajili ya kufunguliwa mashtaka ya jinai. Endapo hatofikishwa mahakamani kwa muda unaopaswa na kuisha, anapaswa kauchiwa na hapaswi kukamatwa tena,” alisema.

Alisema kwa tafsiri hiyo ya kisheria, ni kwamba viongozi wa kisiasa hawazingatii sheria hiyo kikamilifu na ni uonevu mkubwa kwa watumishi waliowekwa ndani.

“Swali la kujiuliza je, uchunguzi ukishakamilika na ikaonekana watendaji waliotangazwa hadharani na kudhalilishwa walionewa, viongozi hao wa Serikali watatumia vyombo vya habari kusafisha majina ya watendaji hao?” alisema na kuhoji.

Mtima alisema kuwa TALGWU haitetei wafanyakazi ambao wanakwenda kinyume na sheria, kanuni na taratibu za kazi, lakini inataka utaratibu ufuatwe na hatimaye watuhumiwa wachukuliwe hatua stahiki.

“Wito wetu viongozi wa kisiasa wenye tabia hiyo watambue dhamana kubwa waliyopewa na Taifa, watumie mamlaka yao kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za nchi vinginevyo kama chama hatutasita kuchukua hatua za kisheria,” alisema Mtima.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles