25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Takukuru yaokoa zaidi ya milioni 11/-

Na JANETH MUSHI-ARUSHA


TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Arusha imeokoa zaidi ya Sh milioni 11.3 ikiwamo zilizokuwa zimelipwa kwa watumishi walioshughulikia maonesho ya Nanenane Kanda ya Kaskazini mwaka 2017.

Baada ya kuokoa kiasi hicho, imetoa taarifa kwa mamlaka inayowahusu kwa ajili ya kuchukuliwa hatua za kinidhamu.

Hayo yalibainishwa mjini hapa juzi na Naibu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Arusha, Frida Wikesi, alipokuwa akitoa taarifa ya utendaji kazi wa taasisi hiyo katika kipindi cha kuanzia Julai hadi Septemba, mwaka huu.

Alisema fedha nyingine zaidi ya Sh milioni 1.2 zilizokuwa za ujenzi wa maabara Shule ya Sekondari Ilkiding’a iliyopo Arumeru zimerejeshwa serikalini.

Kuhusu fedha za Nanenane, alisema watumishi hao wa Serikali walilipwa zaidi ya fedha walizopaswa kulipwa na baada ya kuziokoa walipeleka taarifa kwa mamlaka inayowasimamia ambaye ni Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) wa Arusha ili awachukulie hatua za kinidhamu.

“RAS ndiye amepewa taarifa kuwa kuna idara iliyokuwa inashughulikia maonesho na fedha ambazo zilikuwa na sintofahamu zimeweza kuokolewa, watu walifanya kazi lakini wamelipwa zaidi ya zilizopaswa kulipwa.

“Kama fedha zimeweza kuokolewa na kurejeshwa, wahusika waliosababisha hilo wanachukuliwa hatua za kinidhamu.

“Tunaendelea kudhibiti vitendo vya rushwa kutoa elimu kwa watendaji, wananchi na wadau mbalimbali kwa lengo la kufanya rushwa itambulike kuwa ni hatari na ina madhara makubwa kwa jamii,” alisema.

Pia alisema kipindi hicho cha miezi mitatu wamepokea malalamiko 108 kwa njia mbalimbali kuhusu idara ya ardhi, afya, Nida, kilimo, elimu, Serikali za vijiji na mahakama, huku mashauri 23 yalifanyiwa uchunguzi na kufunguliwa na yako katika hatua mbalimbali za usikilizwaji.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles