Mwandishi Wetu
Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), itatoa elimu kwa wananchi watakaohudhuria Maonesho ya Nanene kuhusu masuala mbalimbali ikiwamo jinsi teknolojia ya nyuklia inavyotumika katika sekta mbalimbali nchini.
Maonesho hayo yanayoanza leo Jumamosi Agosti Mosi, yatafanyika katika Viwanja vya Maonesho TASO mkoani Arusha kwa mikoa ya Kanda ya Kaskazini huku kitaifa yakifanyika kwenye Viwanja vya Nyakabindi, Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa TAEC, Peter Ngamilo amesema teknolojia ya nyuklia inatumika katika sekta ya maji, mifugo, kilimo, viwanda na migodi, hivyo ni fursa ya pekee kuhudhuria katika viwanja hivyo ili kupata elimu juu ya matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia hapa nchini.
Maonesho hayo yamezinduliwa leo kitaifa katika Viwanja vya Nyakabindi na Makamu wa Rais , Samia Suluhu Hassan na yatafungwa na Rais Dk. John Magufuli siku ya kilele Agosti 8, mwaka huu.
Kauli mbiu ya maonesho hayo ni “Kwa Maendeleo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi Chagua Viongozi Bora 2020“.