29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

SULUHU MIMBA ZA UTOTONI NI WAZAZI KUWA WAWAZI

Na Christian Bwaya,

NINGEPENDA kuamini katika mjadala unaoendelea kuhusu mimba za utotoni, kila mtu bila kujali mapendekezo yake anatamani kuona tunamaliza tatizo hili. Hakuna mtu mwenye akili timamu anayeweza kutetea watoto wa kike kupata ujauzito katika umri mdogo.

Ni dhahiri mtoto wa kike anapopata mimba ndoto zake zinayeyuka. Kwa sera zilizopo, kwa mfano, kupata mimba kunamaanisha kupoteza fursa ya kupata elimu. Kukosa elimu katika mazingira yetu kuna maana ya kuandikiwa hukumu ya umasikini.

Lakini pia, mbali na kupoteza fursa ya kuendelea na masomo, watoto hawa wanaopata mimba shuleni wanajikuta katika mazingira magumu linapokuja suala la uhusiano wa kudumu. Wanaume wengi wanaowapa mimba huukwepa mkono wa sheria kwa kuwakataa. Hata wanapokuwa watu wazima, wengi wao hupata tabu kuingia na kudumu kwenye ndoa kwa sababu ya mtazamo hasi wa wanaume wengi.

Kama jamii iliyostaarabika, hatuwezi kuacha hali hii iendelee. Kwanza, tunao wajibu wa kimaadili wa kufikiria namna ya kuwasaidia wasichana wanaojikuta katika mazingira kama haya. Kuwaita wahuni na malaya hakutusaidii sisi wala hakuwasaidii wao. Sambamba na hilo, tunahitaji kutafakari kwa kina namna tunavyoweza kuwaepusha watoto wetu na madhila haya ambayo kimsingi wanajifunza kwetu. Kama tulivyosema katika makala iliyopita, hatuwezi kuwabebesha lawama zote wasichana hawa kwa sababu wanayoyafanya yanafanywa na jamii inayowazunguka.

Katika makala haya tunapendekeza namna nne zinazoweza kutumika kutatua tatizo la mimba za utotoni. Kwanza kabisa, tunahitaji kuelekeza nguvu nyingi katika elimu ya malezi. Tunafahamu kwamba wazazi wengi tumesahau wajibu wetu. Tunapambana na maisha na kuwaacha watoto bila mtu wa karibu anayeweza kujua kinachoendelea katika maisha yao. Tunahitaji kubadili mtazamo wetu.

Wazazi tutambue wajibu wetu. Tujisikie kuwajibika kuwa karibu na watoto tangu wanapokuwa wadogo. Ukaribu huu utasaidia kujenga mawasiliano mazuri yatakayowafanya watoto wawe na imani na sisi. Imani hii ndiyo msingi wa kushirikishwa mambo ya siri yanayowasibu watoto. Bila kuaminika, mzazi hawezi kuwa kimbilio la kwanza mtoto anapokuwa na maswali yanayohitaji majibu.

Kadhalika, tunahitaji kujenga utamaduni wa uwazi zaidi tunapozungumza na watoto. Kuendelea kuyafanya mazungumzo yanayohusu ujinsia na ngono kuwa siri hakuwezi kutusaidia. Mambo yamebadilika. Watoto wanaishi kwenye dunia ambayo taarifa zenye vionjo vya ngono ziko waziwazi. Uholela huu wa taarifa unawafanya wawe na udadisi mwingi. Tukitaka kufanikiwa lazima tuwe tayari kubadilika na kuweka nguvu nyingi kwenye elimu ya afya ya uzazi.

Tunalo tatizo kubwa la watoto wengi kutokujitambua. Wengi wao wanakutana na balehe bila maandalizi yoyote. Hakuna mtu mzima anayethubutu kuzungumza nao. Matokeo yake wanajikuta wakiamini taarifa potofu wanazoziokoteza mtaani na kuzifanyia majiribio. Bahati mbaya, mara nyingi matokeo yake huwa ni kujifunza tabia zilizo kinyume na maadili.

Tuwasaidie watoto kujitambua mapema. Mtoto anapoanza kupevuka mwili, asiachwe akanong’onezwe na wenzake kujua kinachoendelea kwenye mwili wake. Tujenge utaratibu rasmi wa kuwapa elimu inayohusu miili yao. Mifumo yetu ya elimu isiishie kutoa elimu ya afya na uzazi kama nadharia za kukariri kwa ajili ya mitihani. Tuwawezeshe walimu wetu kufundisha masuala haya kwa ufanisi zaidi.

Pamoja na yote hayo, elimu kwa umma ni muhimu. Hivi sasa tunasikia kelele za watu wanaohubiri maadili lakini wao wenyewe wameshindwa kuyaishi maadili hayo. Tunakemea ngono kwa watoto wadogo wakati sisi wenyewe tunawashawishi watoto wadogo kujiingiza kwenye vitendo hivyo. Ikiwa tunamaanisha kukomesha tatizo la mimba za utotoni, tunahitaji kubadilika. Kila mmoja asaidie kuelimisha jamii. Tujisikie kuwajibika kuonesha mfano mwema kwa watoto na wadogo zetu badala ya kuwahukumu kwa kutenda kama tunavyotenda sisi.

Jamii iliyobadilika haitoi hukumu kwa walikosea. Jamii iliyobadilika haimbebeshi lawama mkosefu na kujitenga na wajibu wa kutafuta ufumbuzi. Lawama na kejeli kwa wenye makosa ni ukosefu wa maadili. Hatuwezi kuwa jamii yenye maadili na tukawa tayari kuwakejeli na kuwadhihaki watoto waliopata mimba utotoni. Kipimo cha maadili yetu na ukomavu wetu kama jamii kuwe na namna tunavyofikiria kuwasaidia hata wale ambao tayari wamekosea.

Maadili hayo lazima yatafsiriwe katika sera zetu. Tujiulize, kwa mfano, namna gani sera zetu zinamlinda mtoto na hatari ya kukosa maadili? Namna gani sera zetu zinampa nafasi mtoto aliyekosea kurekebisha makosa yake? Je, sisi kama jamii yenye maadili tunaweza kuwa tayari kuvumilia vitendo vya ngono miongoni mwa wanafunzi wa kiume lakini tukiwafukuza watoto wa kike wanaopata mimba?

Blogu: http://bwaya.blogspot.com, 0754870815

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles