27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

STANDARD CHARTERED MAPATO JUU ROBO YA KWANZA 2017

Na Mwandishi Wetu


Wakati benki nyingi zikihangaika kuishi  na mikopo mingi isiyolipika na mapato kiduchu, ni sherehe kwa Benki ya Standard Chartered Limited ambayo imefanya vizuri katika mapato yake ya robo mwaka  huu kutokana na ubunifu,  kumudu mahusiano mazuri na wateja, kuweko kwa mazao thabiti ya kibiashara na udhibiti gharama  na mikopo kutokana na mwenendo mzuri wa menejimenti.

Benki imeendelea kutoa huduma nzuri ya kuridhisha wateja ambao wameongeza amana zao na kupata faida ya kutosha.

Benki imeendelea kuwa na ukwasi na mtaji stahiki  katika rasilimali zake na kufikia mwishoni mwa robo hii Ukwasi Timilifu wa Benki (Bank Adequacy Ratio) uliishia kuwa asilimia 18 kwa mzingo 1 na  asilimia 20 kwa jumla yote ya mtaji ikifananishwa na mahitaji  ya kikanuni ya asilimia 10 na 12 sawia.

Hayo yaliainishwa na Sanjay Rughani ambaye ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo na kudai mafanikio yamepatikana kutokana na nidhamu thabiti ya utendaji kazi na uzingatiaji maadili mema ya utekelezaji.

“Kadiri tunavyosherekea miaka 100 ya shughuli zetu nchini, mwelekeo ni kuwa ule wa utekelezaji  wa mkakati wetu ambao umejikita katika kuwasaidia wateja wetu kadiri  wanavyokuza na kuendeleza  biashara zao kwa kuanzisha mwenendo mpya wa utendaji kazi  za kibenki  hususani katika matumizi ya sayansi na teknolojia kupitia mitandao.

“Tumezidi kuendelea kuimarisha ushiriki wa kifedha kwa kutumia teknolojia sahihi ya kidigitali iliyoshinda  zawadi  kwa kuendeleza jukwaa la kibenki  kwa wateja wetu wa mtandao na hiyo imetoa msukumo mkubwa kwao. Wateja wetu wameweza kupata huduma zetu za kibenki popote walipo  na wateja  wanaweza wao kufanya mambo ya kibenki huko waliko kwa kufanya miamala ya fedha  bila kufika kwenye sehemu za ofisi zetu kwa kupitia mitandao yetu madhubuti ya kifedha kwa kutumia komputa mpakato zao, iphone  au simu  ya mkononi,” anasema Rughani.

Ruth Zaipuna  ni Mkuu wa Fedha wa Benki ya StanChart, anasema  benki imefanikiwa kupunguza mikopo isiyolipika kutokana na kuwa na mipango thabiti ya ukopeshaji na ulipaji madeni kwa kufahamiana vyema na wateja wao  kwa kuweka mbele masilahi ya pande zote mbili, yaani kwa benki na kwa wateja.

Kwa kuzingatia hayo, benki imeweza kuwekeza katika miradi ya Serikali katika azma yake ya kuifanya kuwa nchi ya uchumi wa viwanda ifikapo mwaka 2025 kwa kufanya maongezi  na watendaji wakuu wa Serikali katika mpango mzima wa viwanda na utekelezaji wake wakiwa na nia thabiti ya kusaidia na kushiriki kikamilifu katika mipango hiyo.

‘Benki ya Standard Chartered Tanzania, kwa mwaka huu ina nia na uwezo wa kutoa fedha kwa Serikali kutekeleza miradi yake iliyopo tayari na ile ambayo iko mbioni kutekelezwa karibuni,” anasisitiza Rughani.

Anasema wana uzoefu kutoka nchi nyinginezo waliko na hivyo kuwa na nafasi nzuri ya kuunga mkono kile ambacho Serikali inafanya au inataka kufanya.

Benki ya Standard Chartered Tanzania inatimiza miaka 100 nchini toka ilivyoanza shughuli zake mwaka 1917 na hivyo imewakirimu zaidi ya maofisa 40 wa ngazi za juu kutoka sehemu mabalimbali duniani hasa Afrika na Mashariki ya Kati waliokuja nchini Machi mwaka huu.

Maofisa hao waliweza kuonana na maofisa mbalimbali wa Serikali na wateja wao wa muda mrefu juu ya uwepo wao nchini  na kusisitiza msimamo wake wa kuendelea kutoa huduma bora.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles