Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital
Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM Taifa, CPA Amos Makalla amesema Soko la kisasa la Chuwini litaleta Mapinduzi makubwa ya kiuchumi kwa wananchi Zanzibar.
Amesema hayo leo Ijumaa Januari 31, 2025 alipokuwa akikagua mradi huo wa kimkakati kwenye muendelezo wa ziara yake ya mikoa sita ya kichama visiwani Zanzibar.
Amesema soko hilo kubwa zaidi ya lile la Kariakoo jijini Dar es Salaam kwani litachukua zaidi ya wafanyabiashara 4,000 kwa wakati mmoja ambapo lile la Kariakoo litachukua wafanyabiashara kati ya 3000-3500.
Aidha amepongeza ubunifu wa kuchanganya soko pamoja na kituo cha mabasi kwa itasaidia sana kukua kwa biashara.

“Nami nijumuike nanyi kuwa kuwapongeza Viongozi wetu Dk. Samia na Dk. Hussein Mwinyi kwa namna wanavyoshirikiana katika kuwaletea maendeleo nilikuwa naona tu kwenye Mitandao nimejionea soko kubwa la kisasa kabisa na kubwa na kupitia hili nimeshawishika kwanini Wajumbe waliamua Dk. Samia na Dk. Mwinyi wawe wagombea wa Urais mapema.
“Kwani hapa mmeweka historia kutoka Bonde la mpunga mpaka soko la kisasa sasa wale Zambarau wenye miwani za Mbao waje wajionee kazi ilivyofanyika kwani kuona ni kuamini,” amesema.