AVELINE KITOMARY – DAR ES SALAAM
WAFANYABIASHARA wa kuku katika soko la Kisutu jijini Dar es Salaam, wamesema hali duni ya upatikanaji wa kuku imesababisha biashara zao kuzorota.
Waliiambia MTANZANIA kuwa tangu kuanza kwa kipindi cha baridi, kumekuwa na uhaba mkubwa wa kuku huku ukuaji hafifu ukiwa chanzo.
Mmoja wa wafanyabiashara hao, Juma Khalifan, alisema kwa sasa bei ya kuku imepanda kutokana Sh 6,000 na kufikikia Sh 7,000.
“Hali ya biashara imeshuka sasa, haijachngamka kama mwanzo, kuku kama ‘broila’ wamepungua, hata ukiangalia mabanda mengi ni makavu, tumekaa tu hapa ilimradi siku ziende,” alisema Khalfan.
Mfanyabiashra mwingine, Abdallah Mkumbo, alisema wameshindwa hata kuendesha maisha yao kutokana na kukosekana kwa kuku.
“Hakuna biashara hapa, kipindi hiki cha baridi kuku huwa hawali chakula kingi na pia hawanywi maji, kwahiyo ukuaji wao unakuwa wa taratibu.
“Kwahiyo tunavumilia kipindi hiki kipite kwani sina biashara nyingine zaidi ya hii ya kuku niliyoifanya kwa muda mrefu,” alisema Mkumbo.
Mwenyekiti wa Soko la Kuku la Kisutu, Zuberi Mtima, alisema licha ya biashara kuwa ngumu kipindi hiki, wafanyabiashara wajitahidi kulipa ushuru wa halmashauri bila kushurutishwa.
“Ni kweli hali ya upatikanaji wa kuku sasa ni ndogo, lakini nawasihi wafanyabiashara wajitahidi kulipa ushuru kwa wakati bila kulazimishwa,” alisema Mtima.