MSANII wa muziki wa Bongo Fleva kutoka Zanzibar, Mustafa Yussuf ‘Smile’, amesema ana matarajio makubwa kuwa juu kisanaa baada ya kuachia nyimbo zake nne alizoshirikiana na wasanii wenye majina makubwa kutoka Bara.
Wasanii alioshirikiana nao katika nyimbo hizo ni pamoja na Emmanuel Eribariki ‘Ney wa Mitego’, Omary Nyembo ‘Ommy Dimpoz’, Elias Brnabas ‘Barnaba boy’ na msanii mmojawapo kutoka kundi la Wasafi ambaye amemficha kama ‘surprise’ kwa mashabiki wake.
Smile anayetamba na wimbo wa ‘Saa ngapi’ aliourekodi studio za Wasafi, aliongeza kwamba lengo la kushirikiana na wasanii hao wenye majina makubwa kwenye muziki wa Bongo Fleva ni kutaka kunyanyua muziki wa Zanzibar na wasanii wake pamoja na kujitangaza kimataifa zaidi.
“Nafikiri wasanii hawa watanifikisha juu kiushindani na hata kugombea tuzo mbalimbali kwa kuwa namna walivyoimba kwa kushirikiana nami, naamini njia yangu ya mafanikio ipo karibu,” alisema Smile.