24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Sitashangaa Azam FC wakimkumbuka Hall

hall-stewart-kocha-wa-azam-fc_1h6rv7amf9jhf1ap090lnyjrqkNA ADAM MKWEPU, DAR ES SALAAM

BAADA ya michezo saba ya Ligi Kuu Tanzania Bara, baadhi ya timu zimekuwa  na furaha huku nyingine zikitafakari makosa waliyofanya na namna ya kufanya maboresho.

Kwa sababu hiyo pia sitoshangaa kuona mashabiki na uongozi wa Klabu ya  Azam FC wakimkumbuka kocha wa zamani wa timu hiyo, Stewart Hall baada ya kuwa na mwanzo mbaya wa michezo ya ligi kuu.

Hadi sasa timu hiyo imepoteza michezo miwili dhidi ya Simba na Ndanda FC kwa kucheza chini ya kiwango, huku ikiwa nafasi ya nne nyuma ya Yanga iliyopo nafasi ya tatu na Stand United ambayo ipo nafasi ya pili.

Wasiwasi ni kuhusu uwezo wa timu hiyo ukilinganisha na vinara wa ligi kuu, Simba ambayo inaonekana kuwa katika kiwango kizuri msimu huu.

Zaidi ni kwamba, Azam FC pia imekuwa ikicheza chini ya kiwango hata katika michezo ambayo imeshinda.

Tangu timu hiyo iwe chini ya kocha Zeben Hernandez, haina uwiano mzuri wa matokeo uwanjani na kama ambavyo ilipokuwa chini ya Mcameroon Joseph Omog au Hall.

Makocha hao ni miongoni mwa waliopelekea mafanikio ya timu hiyo tangu ipande daraja mwaka 2008 huku ikifanikiwa kutwaa ubingwa wa ligi kuu msimu wa 2013/14 ikiwa chini ya Omog na Kombe la Kagame chini ya Hall.

Timu hiyo katika historia yake  imefundishwa na zaidi ya makocha sita baadhi akiwamo Neider dos Santos,  Itamar Amorim, Stewart Hall, Mserbia Boris Bunjak, Joseph Omog na sasa Zeben Hernandez.

Lakini Hall amekuwa kama kocha mlezi wa timu hiyo kwani amewahi kuifundisha kwa vipindi vitatu tofauti huku akitumika kuokoa jahazi linapozama.

Ingawa huenda klabu hiyo ikaona kwamba bado wanatakiwa kuvumilia hali iliyopo, kuna wakati matokeo mabaya yanarudisha nyuma juhudi za klabu ndogo kama za Azam FC kwa kuwa bado inahitaji kuweka rekodi za kutosha ligi kuu na michuano ya kimataifa.

Mashabiki siku zote ushindi ndio kilio chao kikuu hivyo endapo timu itashindwa kuwa na kiwango na matokeo mazuri uwanjani, presha za mashabiki huchukua nafasi yake.

Mchezo wa soka chochote huweza  hutokea kutokana na makosa ndio maana unafahamika zaidi kama mchezo wa makosa, hivyo Azam wanatakiwa kuwa makini kabla ya kupotea kabisa katika timu tatu za juu msimu huu.

Hivyo sitashangaa hata kidogo kama Azam FC itawakumbuka Hall na Omog katika kipindi hiki ambacho ni kigumu kutokana na kusuasua.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles