26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Siri za Mkapa

ANDREW MSECHU -DAR ES SALAAM

KITABU cha Rais mstaafu Benja­min Mkapa, ‘My Life, My Purpose’ (Maisha Yangu, Kusudio Langu), ambacho juzi kilizinduliwa na Rais Dk. John Magufuli, kimeeleza siri za kiongozi huyo wa awamu ya tatu, ikiwa ni pamoja na Mwalimu Julius Nyerere alivyomlimisha kwa saa tatu mara baada ya kumteua kuwa katibu wake.

Kitabu hicho ambacho ni cha kwanza cha aina yake kuandikwa na kiongozi mstaafu wa Tanzania, pia kimeeleza jinsi alivyoandika kimemo kwenda kwa Mwalimu Nyerere kum­weleza nia yake ya kuwania urais.

KULIMA KILA SIKU ASUBUHI

Katika kitabu hicho, Mkapa anasema alianza safari yake ya siasa mwaka 1974, ambapo bila kutarajia, aliteuli­wa kuwa Mwandishi Maalumu wa Mwalimu Nyerere, Ikulu.

Anasema muda mfupi baada ya uteuzi huo, Mwalimu aliondoka kwenda Butiama, hivyo Mkapa alitekeleza majukumu yake kwa ku­kabidhi madaraka ya Mhariri Mtend­aji wa gazeti la Daily News kwa Ferdinand Ruhinda, lakini akiwa na mshangao.

Mshangao wake ulitokana na hatua ya Mwalimu Nyerere kuon­doka kwenda Butiama, akiwa hajui atarejea lini, hivyo aliamua kumfuata.

“Nilimkuta Mwalimu akiwa shambani, alishangaa, akaniuliza ‘Ben, umekuja kunipa taarifa? Ni vye­ma, Karibu’. Nilichukua jembe na ku­ungana naye kwa muda wa saa tatu, suala ambalo lilikuwa gumu kwa mtu aliyezoea kazi za ofisini,” anasema.

Kutokana na hali hiyo, anasema kazi yake ya kwanza baada ya kuteuli­wa kuwa Mwandishi wa Rais ilikuwa ni kulima kila asubuhi, kisha mchana kurejea nyumbani, ambapo Mwal­imu alikuwa akipumzika na kupokea simu, kama sehemu ya mawasiliano na watendaji wake.

“Nilikuwa mwajiriwa wa Ikulu, kwa hiyo nilikuwa makini kujenga uhusiano mzuri na wale niliowakuta pale, akiwemo msaidizi wake, Jo­seph Butiku. Pia nilimfahamu vyema msaidizi wake, Joan Wicken kuto­kana na majukumu yangu,” anasema Mkapa.

Anasema kwa miaka miwili aliyotumikia nafasi hiyo, alisafiri na Mwalimu na kujumuika naye katika vikao vya nchi zilizokuwa mstari wa mbele, ikiwemo Zaire (sasa DR Con­go), Zambia na Botswana.

Mkapa anasema pia alihudhu­ria vikao vya Baraza la Mawaziri la Mwalimu, ambako alijifunza mengi kutoka kwake na kwa mawaziri wal­iokuwa na asili ya India, akiwemo Amir Jamal na Alnoor Kassum.

“Walikuwa wakiuliza maswali mengi sana, walikuwa ni watu wa­naofikiri sana, wenye mitazamo ya kimaendeleo. Waziri Mkuu Msuya (Cleopa David) alinivutia, alikuwa mchapakazi haswa na hakuwa anatu­ingilia kwa kuwa kulikuwa na Wizara ya Habari,” anasema Mkapa.

Anasema Wizara ya Habari wakati huo ilikuwa inahitaji kuunda Wakala wa Habari ambao hatimaye ulithibitishwa na Baraza la Mawa­ziri, kwa hiyo Mwalimu Nyerere al­imwagiza kuanzisha wakala wa hiyo iliyoitwa Shirika la Habari la Taifa (Shihata).

Mkapa anasema baada ya ya hapo, Mwalimu alimtuma kwenda Nigeria ili kurejesha mahusiano mema, kwa kuwa hakukuwa na ba­lozi nchini humo tangu kumalizika vita ya wenyewe kwa wenyewe.

“Uhusiano haukuwa vyema kwa wakati huo kwa kuwa tuliunga mkono wapambanaji wa Biafra wal­iokuwa wakitaka kujitenga, Mwalimu alisema anahitaji mtu anayeweza kuzungumza vyema Kiingereza, ambaye anajua diplomasia, aliyeam­inika na anayeweza kushindana na wahusika.

“Niliwasili Nigeria nikiwa balozi mwishoni mwa Oktoba 1976 na ku­wasilisha nyaraka zangu kwa Jenerali Olusegun Obasanjo ambaye wakati huo alikuwa mtawala kupitia Serikali ya kijeshi,” anasema.

KUTOROKA UBALOZINI

Mkapa anasema baada ya kuteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Ni­geria, mwaka 1976 Mwalimu alifanya ziara ya kiserikali ya siku sita ambayo iilikwenda vizuri, ambapo pia alitoa muhadhara katika Chuo Kikuu cha Ibadan.

Anasema alipoondoka nchini hakuwa amefanya mawasiliano na Wizara ya Mambo ya Nje ili kujua ni mamnbo gani ambayo alipaswa kuyasimamia akiwa nchini Nigeria.

Mkapa anasema wakati huo, al­ilazimika kutoroka baada ya Wizara ya Mambo ya Nje kumkatalia ruhusa ya kuhudhuria uzinduzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho kiliundwa Februari 5, 1977.

“Unajua, nilikuwa mhariri wa gazeti la Chama cha Tanu kwa miaka sita, kwa hiyo hatua ya kuungana kwa Tanu na Afro Shirazi Party na ku­unda chama kipya, ilikuwa muhimu sana kwangu. Halafu mtu ananiam­bia siwezi kuwepo kushuhudia kwa macho yangu. Hilo niliona siwezi kulivumilia,” anaeleza.

Mkapa anasema alimweleza msaidizi wake kwamba aseme taar­ifa iliyotumwa kwa njia ya telegram ikimzuia kurudi nchini, ilifika wakati yeye akiwa ameshaondoka.

Anasema baada ya kuzinduliwa kwa CCM, alizungumza na aliyeku­wa Waziri wa Mambo ya Nje, Ibra­him Kaduma, na wakati huo mtu mmoja aliingia ofisini kwake na kum­wambia kuwa Mwalimu anamuhitaji nyumbani kwake Msasani.

Mkapa anasema alikwenda Msasani, ambako walikuwa wakip­aita kliniki na alipofika, Mwalimu al­imwambia ameamua kumteua kuwa Waziri wa Mambo ya Nje.

Anasema hatua hiyo ilimshtua na Mwalimu alisema anafikiria nam­na ya kumweleza Obasanjo na hajui atalipokea vipi suala hilo.

Mkapa anasema alimweleza Mwalimu kwamba; “Rais wangu, huna haja ya kuhofu kuhusu Obasan­jo, alikupokea vyema wakati wa ziara yako ya kiserikali. Atajua kuwa kuna sababu maalumu ya wewe kuniteua mimi kwa nafasi hii ya juu, kwa nam­na yoyote. Kwa hiyo iwapo utaandika barua nitaiwasilisha mwenyewe na kuitolea maelezo.”

Anasema aliwasilisha barua hiyo kwa Obasanjo na kuwaaga wafan­yakazi wenzake, kisha kurudi Tan­zania kuanza kutekeleza majukumu yake mapya.

KUTENGENEZA FEDHA SI DHAMBI

Mkapa anasema wakati wa utawala wake, miongoni mwa maamuzi magumu aliyochukua ni suala la ubi­nafsishaji, hasa wa viwanda vilivy­okuwa vikimilikiwa na Serikali, mab­adiliko katika utumishi wa umma na kuuza nyumba za Serikali.

Anasema kwa sehemu, ubinaf­sishaji huo ulianza kutekelezwa na mtangulizi wake, Ali Hassan Mwinyi na viwanda muhimu vilivyokuwa vi­kimilikiwa na Serikali ambavyo yeye alisimamia ubinafsishaji wake ni Tan­zania Breweries na Benki ya CRDB.

Mkapa anasema hatua hiyo ili­kuwa muhimu kwa wakati huo kwa kuwa aliamini katika kujitegemea kwa kuwa uchumi wa nchi haukuwa mzuri.

“Elimu ya ujamaa ilikuwa ime­kolea nchini, kuanzia madarasani hadi kwenye Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), mashirika ya umma ilimaanisha kuwa yanamilikiwa na umma, hili lilikuwa limetukaa sana vichwani.

“Hii ilijenga picha kuwa kuten­geneza au kumiliki fedha ilikuwa kosa, haikuwa sahihi. Taasisi ya kiuchumi lazima itengeneze fedha, lakini kwa wale walioamini katika ujamaa hii ili­kuwa kosa.

“Hata sasa unaweza kuona makala za kijamaa katika magazeti au mkufunzi katika chuo kikuu akip­inga ubepari na kuituhumu Tanzania kuwa wakala wa ubepari wa nchi za magharibi,” anasema.

UKOMO WA UONGOZI

Mkapa anasema suala la kubadili­sha madaraka haliepukiki, japokuwa anashangaa baadhi ya nchi za Afrika hazina rekodi nzuri katika suala hili.

Anasema suala hilo limekuwa likivipa vyombo vya habari vya ki­mataifa hasa vya mataifa ya ma­gharibi faida ya bure, kuliko hatua za kubadilishana uongozi kwa njia ya kidemokrasia.

“Ukomo wa urais kwa Tanzania ni vipindi viwili vya miaka mitano mita­no na nakumbuka niliwahi kujadiliana hili na aliyekuwa Rais wa Msumbiji, Joaquim Chissano akasema vipindi viwili havitoshi.

“Anasema katika miaka mitano ya kwanza unaweka miundombinu na kuelewa mifumo inavyofanya kazi, ki­sha unasimamia mipango uliyoiweka kwa manufaa ya taifa, na kwa miaka mitano mingine, inasaidia kusimamia utekelezaji na kuiweka sawa mikaka­ti,” anasema.

Mkapa anasema anadhani awali Chisano alikuwa na mtazamo wa vi­pindi vitatu na huenda alikuwa sahihi, lakini kwa Afrika, watu wana uchu wa madaraka na hadhani kama wa­taruhusu mtu mmoja kukaa madara­kani kwa miaka 15.

“Binafsi, sina tabu na utaratibu wa mihula miwili ya urais, ndiyo maana vipindi vyangu viwili vilipomalizika niliondoka, kuongoza nchi masikini kama hii si jambo jepesi,” anasema.

UDHAIFU WA MWINYI

Mkapa anabainisha kuwa wakati wa utawala wa Rais Ali Hassan Mwinyi, Mwalimu Nyerere alionyesha kutori­dhishwa na utendaji wake, ikiwemo namna alivyosimamia Muungano na kuibuka kwa suala la Serikali tatu.

Anasema katika moja ya kikao walichokaa walijadili suala hilo na yeye akawashauri ni vyema kwanza wakamjuza Nyerere ili kujua maoni yake na alitumwa yeye kwenda ku­peleka ujumbe kwa mwalimu.

Mkapa anasema alitoka kwenye kikao hicho cha Kamati Kuu kilicho­fanyika Dodoma kumpelekea Ny­erere ujumbe huo ambaye alisema; “waambie nimeshatoa maoni yangu kuhusu hilo, suala la muhimu hapa ni kwamba uwaeleze kuwa maoni yangu siwezi kukaa nayo, nitaitisha mkutano wa wanahabari kueleza msimamo wangu.”

Anasema alilazimika kumpigia simu Rais Mwinyi na kumwelekza msimamo wa Nyerere kuwa haungi mkono suala hilo na amepanga kuiti­sha mkutano na wanahabari kutoa maoni yake.

Mkapa anasema baada ya kuzun­gumza naye, Mwinyi aliamua kum­karibisha Nyerere Dodoma kuzun­gumza na Kamati Kuu na aliongozana naye.

“Na alipotoka tu kwenye ndege, niliona baadhi ya watu waliokuwepo wakimwangalia na kusema kuwa yeye (Nyerere) ndiye chanzo cha tatizo.

“Mwalimu alizungumza na Kama­ti Kuu, ambayo baadaye iliamua kuwa na kamati maalumu iliyojumuisha wabunge, wawakilishi kutoka Baraza la Mapinduzi la Zanzibar na Kamati ya Uongozi ya chama, ambapo alizun­gumza nao kuhusu suala hilo la Seri­kali tatu,” anasema.

NJIA YAKE KUWANIA URAIS, DK SALIM KUTAJWA NA NY­ERERE

Katika kitabu chake hicho, Mkapa anaeleza chimbuko la njia yake ya ku­wania urais na jinsi alivyomshirikisha Nyerere na kuibuka jina la Dk. Salim Ahmed Salim.

Mkapa anasema mwishoni mwa mwaka 1994 alijadiliana na mke wake, Anna kuona kama kuna umuhimu kuendelea na siasa.

Anasema baada ya utumishi wa umma uliotukuka kati ya mwaka 1962 hadi 1995, alidhani ulikuwa wakati mwafaka kustaafu shughuli nyingine.

Lakini wakati huo huo, hali ya ki­siasa ilivyokuwa nchini ilimfanya ako­se amani nafsini mwake kutokana na masuala kadhaa kutokwenda vizuri.

Miongoni mwa masuala ambayo yalikuwa yakimsumbua ni hali ya mishahara ya watumishi wa umma, makusanyo ya kodi yalikuwa chini, kulikuwa na sintofahamu kwenye mashirikisho ya wafanyakazi, hasa walimu na washirika wa maendeleo hawakuwa wakifurahia mambo yal­ivyokuwa yakifanyika nchini.

Mkapa anasema baada ya mashauriano na rafiki zake na mke wake, aliona anaweza kusaidia kuwe­ka mambo katika nchi yetu.

“Hatua yangu ya pili ilikuwa kumtaarifu Mwalimu. Nikaandika ujumbe kwenda nyumbani kwake Butiama alipokuwa nikisema; Ndugu Rais, natumaini ni mzima, nimeamua kutafuta kuteuliwa, na nakutumia ujumbe huu kwa sababu sitaki usikie kwa mtu mwingine asije akapotosha juu ya sababu za uamuzi wangu.”

Mkapa anasema alimpa ujumbe huo Joseph Warioba ambaye ni mwenyeji wa mji wa Bunda, mji am­bao ni jirani na Butiama, ingawaje hakumwambia lolote kuhusu kili­chomo kwenye ujumbe, na Mwalimu hakujadili lolote na Warioba kuhusu ujumbe huo.

Mkapa anasema kuwa alikuja kukutana na Mwalimu Nyerere Do­doma, ambako alikwenda kuhudhuria kikao cha Halmashauri Kuu ya cha­ma, na alitumia fursa hiyo kumweleza sababu za kutaka kuteuliwa.

Baada ya kumaliza kumweleza Mwalimu nia yake, alimshukuru kwa kumsikiliza, na kwamba alikuwa msikivu kwa kiwango cha juu, na alimsikiliza bila kutamka neno.

Mkapa anasema baada ya kumal­iza, Mwalimu alimwangalia machoni na kumwambia; “Ahsante sana kwa kuwa mkweli na muwazi kwangu. Nami nitakuwa mkweli kwako.

“Sikuwahi kudhani siku moja utatafuta urais, wazo hilo halijawahi kuja mawazoni mwangu, na si tu kwamba sikutegemea utataka urais, lakini nilikuwa nikifikiria mtu mwing­ine ambaye angekuwa rais bora.

“Lakini juhudi zangu kumshawi­shi hazikufanikiwa, anasita, anadhani anaweza pata uteuzi kwenye sahani, hiyo si siasa, ni lazima upambane. Nilituma mjumbe kwake, lakini hakuonekana kuwa tayari.

“Ben nachoweza kukwam­bia, sitokuzuia, sitakupinga. Kama umeamua, endelea kama dhamira yako inavyokutuma.”

BARAZA LA MAWAZIRI

Mkapa anasema baada ya kuteuliwa na kushinda urais, aliwasiliana na Nyerere ambaye alimpongeza kwa ushindi na alimwomba amsaidie ku­jua ni nani anastahili kuwepo na kwe­nye Baraza la Mawaziri.

Anasema Nyerere alimwambia; “Ben, hili ni baraza lako, siyo langu. Ni Serikali yako, siyo yangu. Kwa hiyo kaa uunde baraza. Ushauri pekee ninaokupa ni kwamba kwanza, tuna makabila mengi, hilo hutakiwi kuli­puuza hilo.

 Jitahidi kuweka usawa, na pili tuna dini nyingi, ila tuna dini kub­wa mbili, hili pia hutakiwi kulipuuza. Zaidi ya hapo, hii ni Serikali yako, ni baraza lako, nenda kaliunde.”

Anasema katika uteuzi wake wa Baraza la Mawaziri, aliamua kuwa wazi na alidhamiria kuwaacha wal­iowahi kuwa mawaziri wakuu, Cleopa Msuya na John Malecela, uamuzi mgumu uliowashangaza wengi.

“Nilikuja kusikia kuwa Mwalimu aliposikia taarifa hizo kuwa wawili waliowahi kuwa mawaziri wakuu si miongoni mwa mawaziri niliowa­teua, alisema hakuwahi kujua kuwa nina maamuzi magumu namna hiyo,” anasema.

WAZAZI WAKE

Mkapa anasema wazazi wake, mmoja alifariki dunia wakati akiwa Waziri wa Mambo ya Nje na mwingine ali­fariki wakati akiwa Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Elimu ya Juu, na kwam­ba kazi yake aliyokuwa akiifanya hai­kuwa chaguo la baba yake, ambaye al­itaka awe kasisi, daktari au mwalimu.

CHIMBUKO LA VUGUVUGU

Mkapa anasema alianza kushiriki katika midahalo na maigizo, akiwa mwanafunzi aliyependa zaidi Hesabu na Kiingereza, ambaye aliwahi kuigiza kama Lady Macbeth katika mashairi ya Shakespear.

Anasema katika midahalo na maigizo alijifunza mambo mengi ambayo baadaye yalimsaidia ka­tika maisha yake ya kazi, hasa katika kuhutubia umma na alipokuwa bun­geni.

Mkapa anasema alikuwa mwa­nafunzi mdogo, lakini machachari katika midahalo hatua iliyomfanya mlezi wao, Father Mc Tiernan kujiku­ta akilazimika kumwambia anyamaze.

“Sikuwahi kuwa na mambo ya kutamani wasichana hadi nilipofika Chuo Kikuu cha Makerere, hata wakati huo ilikuwa kwa mbali sana. Nilikuwa mtu tofauti, mwenye aibu sana kwa wasichana, labda ndiyo maana Father Tiernan alinichagua kuigiza nafasi ya Lady Macbeth,” anasema.

MWAMKO WA KISIASA

Mkapa anasema wakati wa vuguvugu la kudai uhuru, ambapo Chama cha TAA kilibadilishwa jina kuwa Tanu mwaka 1954, alijifunza mambo kad­haa kutoka kwa Mwalimu Nyerere, ambaye aliteuliwa kuwa mwenyekiti wa chama hicho mwaka 1955.

Anasema hatua ya Mwalimu kuji­uzulu na kuacha kazi ya ualimu Pugu kisha kuchaguliwa kuwa mwenyekiti wa Tanu mwaka 1955 iliibua mijadala na mitizamo tofauti baina ya vijana, ambao waliona kuwa ameamua kuwa kama nabii, aliyeamua kuacha ualimu na kuanza safari mpya ya kutumikia taifa lake.

Mkapa anasema darasa la juu wakati huo, mwaka 1955 ambalo lili­kuwa mbele yao, lilikuwa na mwam­ko wa juu wa kisiasa na lilianzisha umajumui wa kisiasa uliopewa jina la ‘Pukka’, naye alikuwa miongoni mwa washiriki waliokuwa na mwamko sana katika jumuiya hiyo.

“Nilikuwa na mwamko sana kati­ka jumuiya hiyo, japokuwa rafiki yan­gu, Oscar Kambona alikuwa akiibeza. Muamko uliokuwepo haukuwafura­hisha walimu wetu na hata matokeo ya GCE yalikuwa si mazuri. Kwahiyo mwaka uliofuata walitusisitiza ku­soma kwa bidii kwa ajili ya mitihani na kuachana na mambo ya siasa,” anasema Mkapa.

Anasema wakati huo alibaini kuwa Waafrika hawana fursa za kuto­sha ikilinganishwa na zile walizokuwa wakizipata watu wa jamii ya waasia na ndipo alipoanza kujitambua, baada ya kuona ofisi nyingi za umma zikiwa zimejazwa waasia na wazungu.

Mkapa anaeleza hapo ndipo al­ipoanza kupata hisia za kukandami­zwa na alianza kuandika barua kwa siri kwenye gazeti la Tanganyika Standard akisisitiza umuhimu wa kujitambua na kudai uhuru, akiwa na miaka 17.

Anasema maendeleo yake shu­leni yalikuwa mazuri kwa kuwa aliku­wa akishika nafasi za juu, ya kwanza hadi ya tatu kati ya wanafunzi 51 na baba yake alikuwa akitamani awe daktari.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles