27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Simba yapiga mkwara, yaahidi kushusha vifaa

Na WINFRIDA MTOI, DAR ES SALAAM

KUELEKEA katika mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara na usajili, Klabu ya Simba imeahidi kufanya mambo makubwa ikijinadi kuchukua mataji yote mawili na kusajili wachezaji wa viwango vya hali ya juu.

Kauli hizo zilitolewa na Ofisa Mtendaji Mkuu wa klabu hiyo, Senzo Mbatha, wakati wa uzinduzi wa tovuti yao mpya jijini Dar es Salaam, jana.

Senzo alisema amekua akiulizwa maswali mengi kuhusu usajili, lakini kwa sasa wanajikita zaidi katika kuhakikisha wanatetea ubingwa wao wa Ligi Kuu na kuchukua taji la Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC). 

Alisema kikosi chao kinatarajia kuanza mazoezi rasmi ya kujianda na michezo yote iliyobaki, kuanzia Jumatano wiki ijayo, huku nyota wao waliopo nje ya nchi wakitarajiwa kutua kabla ya siku hiyo.

“Mashabiki wetu watupe muda na nafasi ili kufanya kazi nzuri kwenye usajili, tutaendelea kufanya kazi na wachezaji waliopo kwa kuwaongezea mikataba mipya, lakini mchezaji yeyote mpya tutakayemsajili tutatoa taarifa.

“Lazima tujikite kwanza kuhakikisha tunashinda Ligi Kuu na FA (Kombe la Shirikisho la Azam), hiyo ndiyo dhamira yetu kuchukua vikombe viwili msimu huu.

“Kabla hatujaanza mazoezi, wachezaji wetu wote watakuwa wamewasili na mmoja wapo kati ya wale waliopo nje Jumatatu (kesho) atakuwa nchini.

“Kuhusu nani anasajiliwa, anayeondoka hayo yatakuja baada ya uongozi kuwasiliana na  benchi la ufundi, lakini sasa Wanasimba tujikite katika Ligi,” alisema Mbatha.

Wachezaji wa Simba waliopo nje ya nchi ni Clatous Chamba (Zambia), Meddie Kagere (Rwanda), Francis Kahata (Kenya) na Sharaf Shiboub (Sudan).

Akizungumzia uzinduzi wa tovuti ya Simba, Senzo alisema ni jambo la kihistoria na lengo ni kutaka klabu hiyo kujulikana kila kona ya dunia.

“Tovuti hii ni ya kisasa, itakuwa imesheheni taarifa zote za Simba ambayo ndiyo klabu kubwa Afrika Mashariki na itakuwa tofauti na tovuti nyingine kutokana na ubora wake,” alisema.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa klabu ya Simba, Haji Manara, alisema imechukua miezi mitano kutengeneza tovuti na kumtaka kila  Mwanasimba aingie kupata taarifa muhimu.

“Hii ni faraja kwa Wanasimba, tumeanza kuitengeneza  tangu Januari na leo (jana) Mei tunaizindua, miongoni mwa vitu vitakavyokuwepo ni hitoria nzima ya klabu na habari mpya za Simba pia itatumia Lugha mbili, Kiswahili na Kingereza,” alisema Manara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles