27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

Simba kuzitumia Coastal, Polisi kuimaliza Namungo

WINFRIDA MTOI-DAR ES SALAAM

MABINGWA wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba,  wamepanga kutumia michezo miwili ya Ligi Kuu Tanzania Bara, watakayocheza dhidi ya timu ya Coastal Union na Polisi Tanzania, kunoa makali yao kwa ajili ya mchezo wa fainali ya Kombe la Shirikisho(FA) maarufu Kombe la Azam dhidi ya Namungo. 

Wekundu wa Msimbazi hao, waliondoka jijini Dar es Salaam jana mchana na kikosi cha wachezaji 22, kwenda Tanga ambako kesho watajitupa Uwanja wa Mkwakwani kuumana na wenyeji wao Costal Union kesho.

Baada ya mchezo huo, mabingwa hao wataelekea mkoani Kilimanjaro ambako Jumapili watakabiliana na wenyeji wao Polisi Tanzania kwenye Uwanja wa Ushirika Moshi.

Ikimalizana na Polisi, Simba iliyoanzishwa mwaka 1935 itakuwa imehitimisha kampeni zake za Ligi Kuu msimu huu hivyo itaelekea mkoani Rukwa kwa ajili ya mchezo wake wa Kombe la Azam dhidi ya Namungo, utakaochezwa Agosti 2 mwezi ujao.

Meneja wa kikosi cha Simba, Patrick Rweyemamu alisema wanataka kushinda michezo yao yote miwili iliyosalia ili kumaliza msimu wakiwa na pointi za kutosha.

 “Baada ya mchezo na Polisi Tanzania ambao utakuwa wa mwisho, tutachukua ndege kutoka Kilimanjaro hadi Mbeya kisha kutumia usafiri wa basi kwenda Sumbawanga.

“Tuna safari ndefu tunapoanza kutoka hapa Dar es Salaam, itahusisha basi na ndege, ina maana Tanga na Moshi, tutatumia basi lakini tukiwa tunaelekea Sumbawanga tutapanda ndege hadi Mbeya, kisha basi kwenda Sumbawanga,” alisema Rweyemamu.

Alieleza kuwa, watatumia michezo yao miwili ya Ligi Kuu dhidi ya Coastal na Polisi kujiandaa na fainali za Kombe la Azam.

“Tuko kamili, malengo yetu ni yale yale hajabadilika, nia yetu tunataka kuchukua Kombe la Shirikisho baada ya kufanikiwa katika ligi, tunawaomba mashabiki na wapenzi, ni kipindi chao cha kufanya yale waliyokuwa wanafanya kuhakikisha wanarejea na kombe hilo,” alisema.

Alisema jana wameondoka na idadi ya wachezaji 22, lakini baada ya mchezo wao na Polisi, wataungana na wachezaji wengine waliosalia Dar es Salaam jijini Mbeya tayari kwa safari ya Sumbawanga.

Kwa upande wake, Nahodha Msaidizi wa timu hiyo, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, alisema wamejiandaa kikamilifu kwa mapambano, lengo likiwa kuendelea kuvuna ushindi na kuwafurahisha mashabiki wao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles