25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

SIMBA, KMC HESABU ZAKUBALI

NA WAANDISHI WETU-BEIRA NA KIGALI

TIMU za Simba na KMC zimechanga vema karata zao, baada ya jana kulazimisha suluhu ugenini, katika michezo yao ya Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho iliyochezwa jana.

Simba ilivuna suluhu hiyo dhidi ya wenyeji UD Songo, katika mchezo wa kwanza wa hatua ya awali wa Ligi ya Mabingwa uliochezwa Uwanja wa Estadio da HCB jijini Beira, Msumbuji.

Kwa upande wa KMC iliibana timu ya AS Kigali,katika mchezo wa kwanza wa hatua ya awali wa Kombe la Shirikisho Afrika uliochezwa Uwanja wa Amahoro jijini Kigali, Rwanda.

Matokeo hayo ni faida kwa wawakilishi hao wa Tanzania, kuelekea michezo yao ya  marudiano itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kati ya Agosti 23 na 25, mwaka huu.

Simba, UD Songo zilivyocheza

Simba itahitaji ushindi ili kutinga raundi ya kwanza ya michuano hiyo, ambapo kama itafanikiwa itacheza na mshindi wa jumla kati ya Nyasa Big Bullets ya Malawi na FC Palatinum ya Zimbabwe.

Simba ilianza taratibu kwa kusoma nyendo za wapinzani, lakini hata UD Songo nao ilicheza kwa kwanza kuepuka kuruhusu bao la mapema.

Dakika ya 13, John Banda alijaribu kumiliki mpira na kuachia mkwaju mkali uliopanguliwa na kipa wa Simba, Beno Kakolanya na kuzaa kona ambayo hata hivyo haikuzaa matunda.

Meddie Kagere alipoteza nafasi ya wazi kuindia Simba bao la kuongoza  dakika ya 18 baada ya kupigiwa pasi safi na John Bocco, lakini aliukosa mpira.

Pachoio Lau Há King alishindwa kutumia vema nafasi aliyopata dakika ya 22, kuindikia UD Songo bao la kuongoza baada ya kupiga shuti lililopita ju ya lango la Simba wakati akiunganisha mpira wa kona.

Kiungo wa Simba, Sharaf Eldin Shiboub alilimwa kadi ya njano dakika ya 26, baada ya kumchezea rafu John Banda.

Nahodha wa Simba, Bocco alishindwa kutumia nafasi aliyoipata dakika 40, kuindikia Simba bao baada ya kuingia na mpira hadi ndani ya eneo la hatari la UD Songo kabla ya kuachia mkwaju uliotoka nje.

Kipindi cha kwanza kilimalizika kwa timu hizo kwenda mapumziko zikiwa zimetoshana nguvu, hata hivyo UD Songo itabidi ijilaumu kwani ilitengeneza nafasi nyingi za kufunga, lakini washambuliaji wake walikosa utulivu wa kutumia.

Simba ilishindwa kuwika kipindi cha kwanza kutokana na kushindwa kucheza kandanda lao la pasi nyingi fupi fupi, baada ya kubanwa hasa sehemu ya katikati ya uwanja.

Hata hivyo, ilitengeneza nafasi mbili ambazo washambualiji wake Kagere na Bocco walikosa maarifa ya kuutia mpira kimiani.

Kipindi cha pili kilianza kwa kocha wa Simba, Patrick Aussems kufanya mabadiliko kwenye safu yake ya kiungo kwa kumtoa Clatous Chama na kumwingiza Mzamiru Yasssin.

Dakika ya 60, UD Songo ilifanya mabadiliko, alitoka Frank Banda na nafasi yake kujazwa na Sebastiano Mario.

Safu ya ulinzi ya Simba ilionekana kufanya makosa ya mara kwa mara,lakini hata hivyo washambulaji wa UD Songo walishindwa kutumia nafasi hizo kujipatia mabao.

Simba ilifanya mabadiliko mengine dakika ya 70, alitoka Francis Kahata na kuingiza Deogratius  Kanda.

Mabadiliko hayo yaliiongozea Simba nguvu kwenye eneo la kiungo na kufanikiwa kutengeneza nafasi nzuri ya bao dakika ya 77, lakini mpira wa kichwa uliopigwa na Shiboub ulipanguliwa na kipa wa UD Songo,Charles Swini.

Dakika ya 78, Aussems alifanya mabadiliko mengine kwenye kikosi chake, alimtoa Jonas Mkude na kumwingiza Hassan Dilunga.

Dakika ya 82, UD Songo ilifanya mabadiliko, alitoka Ernesto Sterio na kuingia Jose Junior.

Dakika ya 90, Jose Junior  wa UD Songo, alilimwa kadi ya njano, baada ya kumchezea rafu Hassan Dilunga.

Katika mchezo huo, UD Songo watajilaumu wenye kwa kukosa utulivu na kushindwa kutumia nafasi nyingi walizotengeneza kwenye mchezo huo.

Hadi dakika tisini zinakamilika matokeo yalikuwa suluhu.

Wakati huo huo, Wawakilishi wa Zanzibar katika Ligi ya Mabingwa Afrika, KMKM iliianza vibaya michuano hiyo, baada ya kukubali kichapo cha bao 1-0 kutoka kwa Primeiro de Agosto ya Angola.

Wawakilishi wengine wa Tanzania katika michuano ya Kombe la Shirikisho, timu ya Azam FC itashuka dimbani leo ugenini nchini Ethiopia kuumana na Kenema.

Kocha Msaidizi wa Azam, Iddi Cheche alisema jana kuwa, wachezaji wake wana morali ya juu ya kutaka kupata ushindi ugenini kabla ya kurejea nyumbani kumaliza kazi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles