27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

SIMBA HAIACHI KITU

Winfrida Mtoi

KAMA ulifikiri Simba imewekeza nguvu Ligi Kuu Tanzania Bara pekee utakuwa unakosea sana kwani, Wekundu hao wamepania kufanya vizuri pia Kombe la Shirikisho(ASFC), baada ya jana kuilaza Stand United mikwaju ya penalti 3-2 na kutinga robo fainali ya michuano hiyo.

Kwakukukumbusha Simba ndiye kinara wa msimamowa Ligi Kuu, ikiwa na pointi 62, baada ya kushuka dimbani mara 24, ikishinda mara 20, sare mbili na kuchapwa mara mbili.

Kabla ya mikwaju ya penalti kutumia kumpata mshindi, dakika 90 za pambano hilo lililopigwa Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga lilikamilika kwa sare ya bao 1-1.

Katika mchezo huo, Stand inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara(FDL)ilionekana kupania kuwabwaga vigogo hao wa Msimbazi kabla ya kukubali kuchemka.

Dakika 45 za kipindi cha kwanza zilimalizika kwa milango ya timu zote kugoma kufunguka.

Simba ilikuwa ya kwanza kufunga bao la kuongoza dakika ya 50, kwa mkwaju wa penalti, uliopigwa na kiungo, Hassan Dilinga, baada ya beki wa Stand, Antidius Ishengoma kuunawa mpira akiwa ndani ya eneo la hatari.

Lakini dakika ya 67, Stand ilisawazisha kupitia kwa Miraj Salehe, aliyepata pasi ya Maulid Fadhil aliyeuwahi mpira uliomponyoka beki wa Simba, Tairone Santos akiwa katika harakati za kuokoa.

Dakika ya sita, Saleh alikosa bao, baada ya  kupata pasi nzuri ilichongwa na Fadhil, lakini alipiga shuti dhaifu lililodakwa na kipa wa Simba, Beno Kakolanya.

Dalika ya saba Shiza Kichuya alishindwa kuiandikia bao la kuongoza Simba licha ya kupokea pasi safi ya Meddie Kagere, baada ya kupiga shuti dhaifu lilidakwa na kipa wa Stand United, Murtala Hamad

Dakika 37, Kagere alikosa bao licha ya kuwa kwenye nafasi nzuri baada ya kupokea krosi ya Kichuya na kupiga mkwaju uliotoka nje.

Pamoja na kila upande kusaka mabao ya ushindi, dakika 90 za pambano hilo zilikamilika kwa sare ya bao 1-1 na ndipo mikwaju ya penalti ilipotumika.

Mshambuliaji wa kimataifa wa Rwanda, Kagere ndiye wa kwanza kupiga penalti kwa upande wa Simba, lakini alikosa baada kiki yake kupanguliwa na Hamad.

Bahati mbaya hiyo ilimkuta pia Ibrahim Ajib wa Simba ambaye mkwaju wake uligonga mwamba wa juu, wakati Clatous Chama, Deogratius Kanda na Hassan Dilunga walifunga kwa upande wa Wekundu hao.

Stand kwa upande mwingine penalti zake   zilifungwa na Fakhi Juma na Brown Raphael, huku Miraj Saleh akikosa kwa kugongesha mwamba kama ilivyokuwa kwa Majid Kimbondile aliyepaisha na Maulid Fadhil iliyopangulia.

Timu nyingine zilizotinga robo fainali ni Sahare All Stars baada ya kuifunga Panama FC  mabao 5 -2 kwenye Uwanja wa Uhuru Dar es Salaam, Namungo FC imeifunga Mbeya City mabao 2-1 Uwanja wa Majaliwa, Lindi.

Ndanda imechomoka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Kitayosa FC kwenye Uwanja wa  Nangwanda Sijaona, Mtwara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles