31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

SIMBA, AZAM MOTO KUWAKA FAINALI KAGAME

Na THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM


TIMU ya Simba imetinga fainali ya Kombe la Kagame, baada ya kuifunga timu ya JKU bao 1-0 katika mchezo wa nusu fainali uliochezwa jana Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.

Boa pekee la ushindi lilifungwa na Meddie Kagere dakika ya 44 na kuihakikishia timu hiyo kucheza mchezo wa fainali ambayo itavaana na Azam FC ambayo iliifunga Gor Mahia mabao 2-0 katika mchezo wa mapema uliochezwa saa 8:00 mchana uwanja huo huo.

Mabao ya Azam yalifungwa na Bruce Kangwa dakika ya 92 huku Ditram Nchimbi akiongeza bao la pili dakika ya 100.

Mchezo wa fainali utachezwa kesho katika Uwanja wa Taifa, Dr es Salaam.

Timu hizo zilianza mchezo kwa kasi kila moja ikionekana kulishambulia lango la mwenzake ili kupata bao la mapema.

Dakika ya 19 mshambuliaji wa Simba, Mohamed Rashid, alishindwa kuisaidia timu yake kupata bao la kuongoza baada ya kupishana na pasi ya Kagere.

JKU ilijibu shambulizi hilo dakika ya 32 kupitia kwa mshambuliaji wao, Ally Hassan, ambaye ilibaki kidogo aipatie timu yake bao la kuongoza lakini shuti lake lilipaa juu ya goli.

Dakika ya 44 Kagere aliwainua mashabiki wa  Simba baada ya kupenyezewa pande akiwa eneo la hatari na Nicholas Gyan na kuachia shuti lililojaa wavuni moja kwa moja.

Timu hizo zilikwenda mapumziko Simba ikiwa mbele kwa bao 1-0.

Kipindi cha pili kilianza huku timu hizo zikiendelea kushambuliana kwa zamu.

Dakika ya 57, Kagere alishindwa kuipatia timu yake bao la pili baada ya  shuti lake kupita pembeni ya lango akiwa ndani ya eneo la hatari akipokea pasi kutoka kwa Marcel Kaheza.

Kosakosa hiyo iliwashtua JKU ambao waliamua kuimarisha eneo la ushambuliaji dakika ya 58 kwa kumpumzisha Ally Vuai na nafasi yake kuchukuliwa na Amour Seleman.

Mabadiliko hayo pia yalifanywa na Simba dakika ya 63 ambayo ilimpumzisha Mzamiru Yassin na nafasi yake kuchukuliwa na Said Ndemla.

Hata hivyo, Simba ilionekana kuwa imara zaidi na kuendelea kuliandama lango la JKU mara kwa mara ikimtumia Kagere kama mshambuliaji wa mwisho.

Dakika 90 za mchezo huo zilimalizika Simba ikishinda bao 1-0.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles