26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Sikonge wazindua zoezi la uogeshaji mifugo

Na Allan Vicent, Sikonge

Halmashauri ya wilaya ya Sikonge mkoani Tabora imezindua zoezi la uhamilishaji na uogeshaji mifugo litakalofanyika katika kata zote 20 na vijiji 71 kwa lengo la kutokomeza magonjwa yaenezwayo na kupe na ndorobo.

Kaimu Mkuu wa Idara ya Mifugo na Uvuvi wilayani Sikonge Mkoani Tabora Mipawa Majebele akionyesha mifugo ya wafugaji wa kata ya Tutuo iliyohusika kwenye zoezi la uhawilishaji (upandishaji madume) na uogeshaji baada ya kuzinduliwa juzi. Picha na Allan Vicent.

 Akizungumza katika uzinduzi huo Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Tito Luchagula amesema zoezi hilo ni muhimu sana kwa kuwa litaokoa mifugo zaidi ya 371,000 yenye thamani ya takribani Sh milioni 185.5.

Ameongeza kuwa zoezi hilo ambalo litagharimu kiasi cha Sh milioni 6.4 litaongeza ubora wa mifugo, uzito na maziwa yanayozalishwa wilayani humo na litawafikia wafugaji wote katika kila kata.

Amesema zoezi hilo litatekelezwa katika kata zote zenye majosho ya kuogeshea mifugo huku akibainisha kuwa wametengea kiasi cha Sh milionini 16 kwa ajili ya ujenzi wa majosho katika kata ambazo hazina miundombinu hiyo.

 “Hii ni fursa muhimu sana kwa wafugaji, naomba kila mtu aichangamkie ili kuboresha zaidi mifugo yetu na kuongeza ubora, uzito na maziwa na hatimaye kuongeza vipato vyetu,” amesema Luchagula.

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Idara ya Mifugo, Mipawa Majebele ameishukuru serikali kwa kuwapatia dawa za ruzuku aina ya Paranex zaidi ya lita 161.5 yenye thamani ya sh mil 6.4 kwa ajili ya kufanikisha zoezi hilo.

“Wafugaji wetu wamekuwa wakijipatia kiasi cha Sh bilioni 24.7 kwa mwaka kutokana na mauzo ya mifugo yao kwenye mnada ambapo halmashauri imekuwa ikipata kiasi cha Sh milioni 180 na serikali kuu Sh milioni 112.

“Pamoja na hayo nakishukuru kituo cha Uhamilishaji cha Taifa kilichoko Arusha (NAIC) kwa kutupatia jumla ya mbegu za ng’ombe 100 zikiwa ni za ng’ombe wa nyama na maziwa, hivyo nitoe wito kwa wakazi wote wa wilaya yetu kuunga mkono juhudi za halmashauri ili kuboresha mifugo yao,”amesema Majebele.

Mkuu wa wilaya hiyo, Peresi Magiri ameitaka halmashauri hiyo kuhakikisha zoezi hilo linatekelezwa kwa ufanisi mkubwa ili kunufaisha wafugaji, aidha aliwataka kuhakikisha miundombinu inajengwa katika kila kata ili kufanikisha zoezi hilo.

Naye, Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Rashid Magope ameishukuru serikali na halmashauri hiyo kwa kufanyia uzinduzi huo katika kata yake ya Tutuo, alisisitiza kuwa zoezi hilo ni muhimu sana kwani litasaidi kuboresha mifugo yao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles